TANZANIA imefaidika katika biashara ya kimataifa, lakini kuna athari ndogo katika utalii na madini kutokana na mtikisiko wa kiuchumi ulioikumba dunia.
Kwa mujibu wa taarifa za utafiti uliofanywa na Benki Kuu ya Tanzania (BoT),Tanzania imefaidika na mtikisiko huo wa kiuchumi kwa biashara ya kimataifa kupanda kutokana na kuporomoka kwa bei ya bidhaa katika soko la kimataifa.
Takwimu za BoT ilizozitoa hivi karibuni pia zimeonesha kuwa mtikisiko huo wa kiuchumi umeleta madhara madogo kwenye utalii na sekta ya madini.
Bot imesema, hadi Septemba mwaka huu, mapato yatokanayo na kusafirisha bidhaa nje yamepanda kwa asilimia 3.2 ikilinganishwa na muda kama huo kwa mwaka jana.
Wakati mapato hayo yakiwa yamepanda kutoka Dola za Marekani bilioni 4.5 hadi dola bilioni 4.6, mapato yatokanayo na kuingiza bidhaa nchini yameshuka na kufikia Dola za Marekani bilioni 7.5 kutoka dola bilioni 7.8 katika kipindi hicho kwa mwaka jana.
Mizania ya biashara ya nchi kati ya mauzo ya nje na bidhaa zinazoingizwa nchini hadi kufikia Septemba mwaka huu, ilipungua kufikia Dola za Marekani bilioni 2.06 kutoka dola za kimarekani bilioni 2.95 kwa mwaka jana katika kipindi kama hicho.
BoT pia ilieleza kuwa gharama za kuingiza mafuta kutoka nje zilipungua kwa asilimia 24.4 kufikia Dola za Marekani bilioni 1.3 katika mwaka huu unaoishia Septemba.
Kwa mujibu wa BOT,hali hiyo inatokana na kuanguka kwa bei ya mafuta katika soko la dunia ingawa kiwango cha mafuta kilichoingizwa nchini kiliongezeka kwa tani milioni 2.2 mwaka jana hadi kufikia tani milioni 2.9 mwaka huu.
Mkuu wa utafiti wa uchumi na sera wa BoT, Joe Massawe alisema, “licha ya kutokea matatizo ya kiuchumi nchini, kushuka kwa bei ya bidhaa katika soko la dunia kumesababisha kushuka kwa gharama za kuagiza bidhaa kutoka nje. Hii pia imepunguza gharama za uzalishaji.”
Wakati huo huo, Mkuu wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) nchini, David Robinson alisema hali ya kiuchumi nchini ni nzuri wakati huu wa mtikisiko wa kiuchumi duniani na hali hiyo imetokana na Tanzania kutoingiliana sana na uchumi wa kimataifa