Wajenga uwezo Afrika wapiga tafu Afrika Mashariki Imeandikwa na Anastazia Anyimike; Tarehe: 25th July 2010 @ 23:30 Imesomwa na watu: 229; Jumla ya maoni: 0
TAASISI ya Kujenga Uwezo ya Afrika (ACBF) imetoa jumla ya dola za Marekani milioni 2.3 kwa taasisi mbili kwa lengo la kuzisaidia kukuza uchumi na kusaidia maendeleo ya mafunzo mtandaoni.
Taasisi zilizonufaika na fedha hizo ni Baraza la Biashara la Afrika Mashariki (EABC) lililopewa dola za Marekani milioni 1.8 (zaidi ya shilingi bilioni 2.5) na Kituo cha Maendeleo ya Mafunzo ya Mtandao (TGDLC) ambacho kimetenga dola za Marekani 500,000 sawa na zaidi ya Sh milioni 700.
Akizungumza wakati wa kutia saini makubaliano hayo yaliyofanyika juzi, Katibu Mtendaji wa ACBF, Dk Frannie Leautier alisema makubaliano ya EABC ni kwa miaka minne wakati yale ya TGDLC ni kwa miaka mitatu.
“Makubaliano hayo kwa EABC yamekuja muda muafaka wakati kumeshaanza kutekelezwa kwa makubaliano ya Soko la Pamoja la nchi za Afrika Mashariki ambalo linatoa uhuru wa maingiliano katika mitaji, ajira, bidhaa na huduma hivyo kuwa na mahitaji kwa sekta binafsi kutoa huduma na bidhaa bora."
“ACBF itahakikisha inalisaidia baraza kutimiza programu zao, kwa lengo la kujenga uwezo katika sekta binafsi katika Jumuiya ya Afrika Mashariki na pia TGLDLC kwa lengo la kutekeleza mradi wa Tanzania Country Level Knowledge Network (TZ CLK-NET),” alisema.
Aidha, Mwenyekiti wa Bodi ya TGDLC, Florens Turuka alisema kuwa fedha hizo zitasaidia kukuza na kuendeleza mtandao wa mawasiliano hapa nchini.
Mgeni rasmi katika hafla hiyo, Naibu Katibu Mkuu wa Sekretarieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Alloys Mutabingwa pamoja na kuishukuru ACBF kwa kutoa fedha hizo, alisema msaada huo utasaidia kujenga mazingira bora ya biashara kwa nchi wanachama wa jumuiya hiyo.