Wachakachuaji mikopo kukiona
- Imeandikwa tarehe 14 Septemba 2012
- By Mwandishi Wetu
- Imesomwa mara: 354
MFUMO wa kukusanya na kutunza kumbukumbu za wakopaji, uko tayari na Benki Kuu ya Tanzania (BoT) inatarajia kuuzindua Septemba 28, mwaka huu.
Gavana wa Benki Kuu, Profesa Benno Ndulu alibainisha hayo wakati Waziri wa Fedha, Dk William Mgimwa alipotembelea Makao Makuu ya BoT jijini Dar es Salaam juzi.
Kwa mujibu wa Profesa Ndulu, mfumo huo utaweka bayana taarifa za wakopaji kwa pande zote mbili, yaani baina ya wakopaji na wakopeshaji (mabenki).
Aliongeza kuwa tayari kampuni moja ilikuwa imeshapewa leseni ya kufanya kazi hiyo wakati mchakato wa kuipatia leseni kampuni nyingine ya pili ulikuwa ukiendelea.
Kwa mujibu wa taarifa ya Idara ya Uhusiano wa Umma na Itifaki ya BoT, Profesa Ndulu alisema benki za jamii sasa zitahitajika kuwa na mtaji wa Sh bilioni 2 badala ya kiwango cha awali cha Sh milioni 250.
Alisema kwa kufanya hivyo, bila shaka kutakuwa na changamoto za kisiasa, lakini akaongeza kwamba ilikuwa ni muhimu kwa benki zote za jamii kuwa na fedha za kutosha ili zimudu kujiendesha kwa ufanisi zaidi.
Pia alisema kulikuwa na mpango wa Benki Kuu kuachia baadhi ya shughuli inazozifanya sasa hivi ili itilie mkazo kazi zake za msingi.
“Kazi hizo ni pamoja na usimamizi wa mifuko ya udhamini wa mikopo na usimamizi wa madeni, ambapo kuna mwelekeo wa kuzihamishia Hazina,” alisema Profesa Ndulu.
Awali, Dk Mgimwa ameiunga mkono Benki Kuu katika kutilia mkazo utendaji wa kazi zake za msingi ili itekeleze majukumu yake kikamilifu zaidi kwa faida ya nchi.
Hii ilikuwa ni mara ya kwanza kwa Waziri kuitembelea Benki Kuu tangu alipoteuliwa kushika wadhifa huo na Rais Jakaya Kikwete, Mei mwaka huu. Katika ziara hiyo, Dk Mgimwa alifuatana na mmoja wa manaibu wake, Saada Mkuya Salum na maofisa wengine waandamizi wa wizara hiyo.
Mkutano huo ulihudhuriwa na Profesa Ndulu na naibu Gavana wake wawili, Lila Mkila (Uthabiti wa Sekta ya Fedha), Dk Natu Mwamba (Uchumi na Sera za Fedha) na Menejimenti ya Benki Kuu.
Dk Mgimwa alisifu kazi nzuri inayofanywa na Benki Kuu na hasa katika kuhakikisha kuna ukwasi wa kutosha wa fedha, akiongeza kwamba juhudi hizo sharti zidumishwe ili kuiwezesha sekta ya fedha kuwa salama.
Alisema ni jambo muhimu kwa benki zote kuwa na fedha za kutosha kwani hali hii inazifanya benki kuwa na uwezo wa kutoa huduma mbalimbali ikiwa ni pamoja na kutoa mikopo kwa wananchi.
“Kwa maana hiyo, uamuzi wa Benki Kuu kuzitaka benki zote za biashara kuwa na mtaji wa fedha kiasi kisichopungua Shilingi bilioni 15 ilikuwa ni hatua nzuri,” alisema Dk Mgimwa. Uamuzi huo ulifikiwa na Benki Kuu Juni 2010.
Hali kadhalika, Dk Mgimwa aliitaka Benki Kuu kutoa maagizo kama hayo kwa asasi nyingine ndogo ndogo zinazotoa huduma ya fedha ili kusudi uendeshaji wa shughuli zake uwe wa uhakika zaidi.


