24Mei2013

 

Balozi Sarakikya aipa somo TTB

MKUU wa Majeshi mstaafu, Balozi Mirisho Sarakikya ameitaka Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), kutumia mabalozi wa nchi mbalimbali waliopo nchini pamoja na marafiki zao kupanda Mlima Kilimanjaro kila mwaka kama sehemu ya kutangaza utalii wa ndani na nje.

Amesema mara kadhaa akiwa Balozi wa nchi za Ethiopia, Nigeria na Kenya alikuwa akiandaa safari kwa mabalozi wa nchi mbalimbali kwa ajili ya kupanda mlima huo jambo ambalo lilisaidia kwa asilimia kubwa kuutangaza mlima huo.

“Tuache kulalamika, wenzetu wa Kenya walikuwa wanasema njoo Kenya uone Mlima Kilimanjaro….hiyo si sahihi lakini na sisi tutumie fursa hiyo kusema njoo Tanzania upande Mlima Kilimanjaro, mabalozi hawa wana nafasi ya kukuza utalii wetu,” alisema.

Jenerali Sarakikya ambaye amepanda mlima huo mara 38, alisema hayo wakati akizindua safari ya Kamati ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira sanjari na viongozi mbalimbali wakiwemo wanajeshi kupanda mlima huo kwa Lango la Marangu, Moshi Vijijini.

Wabunge wanaoongozwa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, James Lembeli aliyeambatana na Makamu Mwenyekiti, Abdulkarim Shah, Meshak Opulukwa, Mariam Kasembe, Amina Clement na Josephat Kandege.

Sanjari na mabalozi hao, Jenerali huyo aliishauri Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki kuunda chombo maalumu kitakachojumuisha raia wa nchi hizo, ili pamoja na kujenga uhusiano wa karibu lakini hatua hiyo pia isaidie kuutangaza mlima huo.

Alisema safari ya kupanda mlima kwa kipindi chote alichoshiriki, kumekuwepo na mabadiliko ya aina mbalimbali, ikiwamo ujenzi wa vyoo na usafi wa mazingira jambo ambalo hapo awali halikuwepo na watalii walikuwa wakijisaidia vichakani.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Hifadhi za Taifa (TANAPA), Alan Kijazi, katika taarifa iliyosomwa kwa niaba yake na Mkurugenzi wa Hifadhi na Ikolojia wa shirika hilo, Martin Loibook alisema wanatarajia kupokea mapendekezo kutoka kwa wabunge hao jinsi ya kuboresha mazingira.

Mapema akizungumza katika safari hiyo inayoongozwa na Mkuu wa Majeshi mstaafu, George Waitara, Mwenyekiti wa Kamati hiyo ya Bunge, James Lembeli, alisema atakwenda kushawishi kamati nyingine kupanda mlima huo ili kuutangaza.