Taasisi ya Wahandisi yaonya kuhusu uchumi
- Imeandikwa tarehe 04 Machi 2013
- By Mwandishi Wetu
- Imesomwa mara: 251
KUKUA kwa uchumi wa Tanzania kutazidi kupata vipingamizi, endapo Serikali haitachukua hatua madhubuti za kuwajengea uwezo wahandisi wazalendo.
Tahadhari hiyo imetolewa na Taasisi ya Wahandisi Tanzania (IET).
Tahadhari hiyo ilitolewa na wahandisi waliohudhuria mkutano wa wahandisi ulioandaliwa na taasisi hiyo, kujadili umuhimu wa wahandisi katika utatuaji wa changamoto zinazoikabili na kuwa kikwazo kwa maendeleo ya kiuchumi, zikiwepo ajira, elimu, ukiukwaji wa taratibu zinazoendana na fani ya uhandisi na matumizi mabaya ya rasilimali.
Akizungumza wakati wa mkutano huo, Rais wa Taasisi ya Wahandisi Tanzania, Dk Malima Bundara alisema changamoto zinazoikabili sekta ya uhandisi nchini itapatiwa ufumbuzi endapo uhusishwaji wahandisi wa ndani utapewa kipaumbele.
“Sekta ya uhandisi inakabiliwa na changamoto nyingi lakini zitaweza kupatiwa ufumbuzi endapo wahandisi wazalendo watahusishwa katika kutatua matatizo hayo,” “Tusijidanganye kuwa wahandisi wa kigeni watatoa ufumbuzi wa muda mrefu wa matatizo tuliyonayo kama nchi. Hawa wamekuja kutafuta pesa na kurudi nazo kwao.
Tunatakiwa kuwajengea uwezo wahandisi wetu wa ndani, ambao watatoa majibu ya changamoto zinazokabili miundombinu yetu ambayo inaathari katika uchumi wa nchi,” alisema.
Bundara aliitahadharisha Serikali dhidi ya kuacha kuwatumia wahandisi wazalendo katika utafutaji wa ufumbuzi wa changamoto zinazorudisha nyuma maendeleo zinazoikabili nchi.
Aliwataka wahandisi wazalendo waachane na kulalamika, badala yake wachukue hatua ili kusaidia kukuza uchumi wa Taifa. “Nguzo ya ukuaji kwa uchumi katika kila nchi ni upatikanaji wa miundombinu imara na inayoeleweka.
Maendeleo ya miundombinu na kukua kwa sekta ya viwanda ipo mikononi mwa wahandisi. Kama Serikali na taasisi zake itawatumia vizuri wahandisi wazalendo, mapinduzi ya haraka katika uchumi wa nchi yatapatikana,” alisema Bundara.
Aidha, alibainisha kuwa taasisi ya wahandisi Tanzania imejipanga kutekeleza mpango wake wa kuwajengea uwezo wahandisi wa ndani ili kuwapatia mbinu za kitaalamu katika masuala yanayowalenga katika fani, ambayo pia yanaathiri moja kwa moja uchumi wa nchi.
Kwa upande wake, Rais wa zamani wa Taasisi hiyo, Ladislaus Salema alishangaa ni kwa nini nchi iliyobarikiwa kuwa na rasilimali na maliasili za kutosha kama Tanzania, bado inapata shida katika utengenezaji wa ajira kwa wananchi wake na bado imeorodheshwa katika nchi zinazoendelea.
Aliiasa Serikali inahitaji kufanya kazi kwa karibu na wahandisi katika jitihada za kukwamua Taifa katika janga la ukosefu wa ajira.
Mwanachama wa taasisi hiyo, Shabbir Khataw aliwaonya wahandisi wenzake dhidi ya uzembe, na kusema kuwa baadhi ya wahandisi wanaohitimu vyuo vikuu hupenda kukaa maofisini badala ya kufanyia mazoezi ujuzi wao, tabia ambayo inawanyima nafasi ya kuongeza ujuzi wao.




