21Mei2013

 

Bodi kuratibu taaluma ya ualimu

SERIKALI inaanzisha Bodi ya Kitaalamu ya Walimu katika mwaka huu wa fedha kwa ajili ya kusimamia na kuratibu taaluma ya ualimu.

Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa alisema hayo jana wakati akiwasilisha bungeni makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka 2012/13. Wizara imeomba iidhinishiwe Sh 724,471,937,000 ili kutekeleza majukumu yake.

Waziri Kawambwa ambaye alikuwa akielezea malengo ya bajeti mwaka huu katika Idara ya Elimu ya Ualimu, alisema Bodi hiyo itaanzishwa kupitia idara husika.

Katika kuelezea malengo mengine yatakayofanyika katika idara hiyo, Dk Kawambwa alisema pia wataanza kutumia Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE) katika kudhibiti ubora wa elimu ya ualimu.

Akizungumzia malengo mengine ya wizara katika Idara hiyo ya Ualimu, alisema itaingiza na kutunza kumbukumbu za watumishi, wanachuo na mali za vyuo vya ualimu katika mfumo wa kielektroniki.

Alisema pia wizara itafanya ufuatiliaji, tathimini na mapitio kuhusu utekelezaji wa mkakati wa menejimenti ya maendeleo ya walimu.

Pia itaendesha mafunzo ya ‘waelimisha walimu’ kwa wakufunzi 580 wa vyuo vya ualimu vya Serikali ili kuwajengea uwezo wa kuendesha mafunzo husika kwa ufanisi.

Mkakati mwingine ni wa kudahili wanachuo 11,545 wakiwamo 5,770 wa ngazi ya Cheti na 5,775 wa Stashahada na kufanya jumla ya wanachuo wote katika vyuo vya ualimu vya Serikali kuwa 26,800. Kati ya hao, 180 watasomea namna ya kufundisha watoto wenye mahitaji muhimu.

Aidha, itatoa mafunzo kwa wakufunzi 180 ili kuimarisha matumizi ya Tehama kama mbinu ya kufundishia na kujifunzia.

Itatoa mafunzo kazini kwa walimu 420 wa shule za msingi na sekondari pamoja na wakufunzi wanaofundisha masomo ya Sayansi, Hisabati na Kiingereza.

Katika hatua nyingine, Dk Kawambwa alisema wizara itaendelea kusimamia na kuimarisha michezo katika vyuo 12 vya ualimu vya Serikali kwa kushirikiana na Shirika lisilo la Kiserikali la LIIKE la Finland. Vile vile itaanza utekelezaji wa mkakati wa mafunzo ya ualimu kazini-Elimu ya Msingi (Mwakem) kitaifa.