22Mei2013

 

Wananchi wataka Serikali ya Tanganyika

BAADHI ya wananchi waliopata fursa ya kutoa maoni mbele ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba mkoani Katavi wamependekeza kurejeshwa kwa Serikali ya Tanganyika.

Kwa kipindi cha zaidi ya wiki moja ambacho gazeti hili limefuatilia maoni ya wananchi wa vijijini, wananchi hao walisema kuwa umefika wakati Serikali ya Tanganyika irejeshwe na hivyo Muungano utakaokuwepo katika Katiba mpya, uwe wa serikali tatu.

Ni wananchi wachache ambao walitaka kuwepo kwa Serikali moja ya Tanzania na kufutwa kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) kwa maelezo kuwa muundo wa serikali mbili ndio uliosababisha Wazanzibari kuleta chokochoko ya kutaka kujitenga.

Mkazi wa Kijiji vya Usevya, Joakim Marema alisema zamani kulikuwepo na Serikali ya Tanganyika, ikauawa baada ya kuungana na Zanzibar lakini upande wa pili wa Muungano haukuwa kama ilivyotokea kwa Bara.

“Umefika wakati Serikali hiyo (Tanganyika) irejeshwe na Muungano uwe wa serikali tatu,” alisema Marema.

Naye Mwita Matiko alisema inaonesha kuwa Bara ndio inaowabembeleza Wazanzibari kwenye Muungano kwani lugha wanazotoa zinaashiria kuwa hawataki Muungano, lakini akashauri ili kumaliza mvutano uliopo, ni vyema ziwepo serikali tatu.

“Hawa wenzetu ni wabinafsi maana walivyogundua mafuta tu wakatangaza kuwa hayawezi kuwa ya Muungano, lakini kwa kipindi kirefu wametumia rasilimali za Bara na sisi hatujalalamika, nadhani na sisi tuwe na serikali yetu,” alisema.

Mkazi wa Kijiji cha Majimoto, Issa Mgheni alisema serikali tatu kwa sasa ndio jawabu na akaonya kuwa iwapo tume hiyo itapuuza maoni mengi ya wananchi na kutaka kuendelea kwa Serikali mbili, kuna hatari ya Muungano huo kuvunjika.

Rehema Mwakalolo yeye alisema serikali tatu ziwepo lakini ziwe chini ya Rais mmoja na mawaziri wakuu wawili ambao mmoja ataongoza Serikali ya Tanganyika na mwingine ataongoza Serikali ya Zanzibar.

“Na sisi tunataka serikali yetu kwani Wazanzibari wana serikali yao, bendera yao na mambo mengi wanafanya kuelekea kwenye Dola huru, ni nini sasa kinatunyima sisi haki ya kuwa na taifa letu?” Alihoji Rehema.

Alifafanua kuwa nchi moja ikiwa na marais watatu, yaani wa Muungano, Tanganyika na Zanzibar, Katiba itengenezwe ili serikali mbili za kila upande ziongozwe na mawaziri wakuu ambao wataunda serikali zao na Rais wa Muungano naye aunde serikali ndogo.

Nikansi Kapala wa Kijiji cha Mamba, alisema Serikali tatu kwa sasa hazikwepeki na akasisitiza kuwa Muungano wenye serikali hizo utakuwa imara kwani kila upande utamiliki rasilimali zake.

Alipendekeza mambo machache tu ndio yaingizwe kwenye Muungano kutoka 22 ya sasa na yabaki ya Mambo ya Ndani, Jeshi la Ulinzi pamoja na Wizara ya Mambo ya Nje. Tathmini ya wiki moja imeonesha kuwa wale wanaotaka Muungano wa serikali moja, wanasema kuwa siku zote vitu viwili vinavyoungana ni lazima vizae kitu kimoja na sio tena vitu viwili.

“Kwenye ndoa mume na mke wakiungana wanakuwa mwili mmoja, iweje nchi hizi ziungane zibaki serikali mbili, haiji akilini tuwe na nchi moja tu,” alisema Godwin Kalawa.

Wananchi waliopendekeza serikali mbili, walisema ndio mfumo mzuri wa kuendelea kuleta amani kwa Tanzania kama ilivyo sasa.