Tutahakikisha elimu inaendelea kukua-Dk Kawambwa
- Imeandikwa tarehe 14 Septemba 2012
- By Mwandishi Wetu, Arusha
- Imesomwa mara: 428
SERIKALI imezihakikishia taasisi za elimu ya juu nchini kuwa itaendelea kuweka mazingira mazuri ya kisera na kuhakikisha elimu inaendelea kuwa chachu kubwa kufikia Dira ya Maendeleo ya Nchi ya 2025.
Haya yalisemwa na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa wakati wa Kongamano la Nne la Elimu ya Juu jana jijini Arusha.
Kongamano hilo linalomalizika leo limetayarishwa na Kamati ya Makamu Wakuu wa Vyuo Vikuu na Wakuu wa Vyuo Tanzania (CVCPT) kwa kushirikiana na Taasisi ya Trust Africa. Kaulimbiu ya Kongamano hili ni Utawala Bora kwa Elimu Bora Endelevu ya Vyuo Vikuu Tanzania.
“Hakuna nchi inayoweza kujipatia maendeleo makubwa bila kuwa na idadi ya kutosha ya wasomi katika nyanja mbalimbali,” alisema Dk Kawambwa aliyekuwa mgeni rasmi katika kongamano hilo.
Alisema ili mahitaji ya rasilimaliwatu na Dira ya Maendeleo ya Kitaifa ifikapo mwaka 2025, nchi haina budi kuzalisha walau wahitimu 80,000 kutoka katika vyuo vikuu.
Alisema kwa juhudi za Serikali imewezekana kuongeza idadi ya wanafunzi wanaojiunga na vyuo vikuu kwa asilimia 19 kutoka wanafunzi 139,638 mwaka 2010/2011 hadi 166,484 mwaka 2011/2012.
“Hii imetokana pamoja na mambo mengine kwa sababu ya ongezeko la vyuo kufikia 46 hapa nchini,” alisema Dk Kawambwa na kuongeza kuwa kutekeleza utawala bora ni changamoto, lakini suala hilo lazima lifanyike kwa maendeleo ya uchumi wa nchi.
“Ni lazima utawala bora utekelezwe katika vyuo vikuu, sio kwa maneno tu, bali kwa vitendo,” alisema.
Mwenyekiti wa CVCPT, Profesa Joseph Kuzilwa alisema majadiliano ya kongamano hilo yataleta maazimio yanayofaa ya kisera katika kuendesha vyuo vikuu na hivyo kuchangia zaidi katika maendeleo ya nchi.
Chuo Kikuu Mzumbe kama Mwenyekiti wa sasa wa CVCPT, kimepewa jukumu kwa niaba ya CVCPT kuwa mwandaaji wa kongamano hili.
Kwa mujibu wa Profesa Kuzilwa, malengo ya kongamano hilo ni kutathmini ubora wa mifumo ya utawala na kuangalia ni kwa kiasi gani inakwamisha utawala bora katika vyuo vikuu, kuangalia changamoto zinazovikabili vyuo vikuu na namna gani utawala bora unaweza kutatua changamoto hizo na kuanzisha mikakati ya pamoja kwa ajili ya kuimarisha utawala bora katika vyuo vikuu.



