21Mei2013

 

Wanaotaka kumng’oa Ndalichako waonywa

WAKATI kikundi cha Waislamu leo kikitarajia kuandamana katika vikundi vidogo kwenda Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA) kumwondoa Katibu Mkuu wa Baraza hilo, Dk Joyce Ndalichako, Polisi imetoa onyo dhidi ya kikundi hicho.

Taarifa zilizopatikana jana zilieleza kuwa kundi la Jumuiya na Taasisi za Kiislamu lililo chini ya Shehe Ponda Issa Ponda, limepanga kuandamana hadi Nacte kushinikiza uongozi wa Baraza hilo kujiuzulu kwa madai ambayo yalishatolewa ufafanuzi na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi.

Mkurugenzi wa Taasisi ya Tanzania Islamic Peace Foundation (TIPF), Shehe Sadik Godigodi alisema jana, kuwa wamepata taarifa hizo na kutoa mwito kwa Waislamu kutoshiriki maandamano hayo yaliyopangwa kufanyika kama ilivyokuwa wiki iliyopita walipokwenda Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Shehe Godigodi alisema nchi haiwezi kuendeshwa kwa utashi wa kikundi ambacho nyuma yake kuna shinikizo la kisiasa kutoka chama cha siasa, ambacho Mwenyekiti wake hivi karibuni alifanya ziara misikitini.

Alidai pia kuwa Mwenyekiti wa chama hicho alikuwa mgeni rasmi kwenye Baraza lao la Iddi lililofanyika Mwembeyanga, Temeke. “Tunaomba Waislamu nchini kuchukua hadhari dhidi ya kikundi hiki ambacho hakina nia njema na nchi hii, pia tunaomba Serikali kuwa makini na vikundi kama hivi na kuacha tabia ya kuvilea,“ alisisitiza Shehe Godigodi.

Alisema tayari kasoro ya usahihishaji wa somo la Kiislamu kwa alama ya mwisho kugawanywa kwa tatu badala ya mbili ambayo ndiyo idadi sahihi ya karatasi za somo hilo kuanzia mwaka huu, limeshatatuliwa, hivyo hakuna sababu ya kuandamana.

“Tunaamini kuwa wahusika wote walijulishwa kuhusu dosari hiyo na marekebisho yalifanyika kama ilivyotakiwa, sasa inashangaza kuwa suala hilo limetoka wapi baada ya kumalizika la sensa?”Alihoji.

Alisema Serikali haina dini na kuhadharisha kwamba wasidhani Wakristo hawawezi kuandamana na wala si kwamba wanaridhika na hilo, bali wamekuwa watiifu kwa Serikali iliyoko madarakani.

Kova aonya Wakati huo huo, Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam imeonya mtu au kundi lolote linalopanga njama za kutaka kumwondoa madarakani kwa nguvu na kwa kutumia mabavu, Mufti wa Tanzania, Shehe Mkuu Issa bin Shaaban Simba na viongozi wake au kuvamia Necta.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam, Kamanda wa Polisi wa Kanda hiyo, Suleiman Kova alisema wamepokea malalamiko rasmi kutoka Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA), na wanayafanyia kazi kwa kuwa jukumu la Polisi ni kulinda usalama.

"Tumepokea malalamiko rasmi na kufungua jalada la kesi kuhusu tuhuma hizo ambazo lengo lake ni kutumia nguvu na mabavu katika hali inayoashiria uvunjifu wa amani... ni jukumu la Serikali kupitia vyombo vya Dola kuhakikisha uwepo wa usalama wa taasisi yoyote iliyosajiliwa kisheria kama ilivyo Bakwata," alisema.

Alisema ni wajibu wa Jeshi hilo kulinda viongozi walioko madarakani mpaka taratibu za kiutawala na kikatiba zitakapowaondoa madarakani.

Alisema watu 10 watahojiwa kutokana na tukio hilo ambapo hadi jana watu wawili ambao hakuwataja majina kwa sababu za kiusalama, walikuwa wakiendelea kuhojiwa na kuwataka wengine kujitokeza kabla ya kukamatwa.

"Ni lazima ifahamike wazi kuwa Jeshi la Polisi halitasita kuchukua hatua madhubuti za kisheria pale kundi lolote la kidini, kisiasa au taasisi yoyote itakapobainika kuhatarisha usalama wa wananchi wasio na hatia," alisema.

Alisema anauhakikishia uongozi wa Bakwata kwamba Polisi iko makini na hatua zinaendelea kuchukuliwa kukabiliana kikamilifu na kundi dogo au kubwa litakalojaribu kuvamia ofisi za Bakwata, Necta au mamlaka nyingine yoyote.

"Tunawasihi wananchi au wafuasi wa vikundi hivyo ambavyo si rasmi, wasifuate mkumbo katika kutekeleza azma hiyo, kwani yeyote atakayeshiriki atakamatwa na kuchukuliwa hatua kali za kisheria mara moja," alionya Kova.

Naye Halima Mlacha anaripoti kwamba Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi imemsimamisha kazi na itamchukulia hatua za kinidhamu Mkuu wa Idara ya Utafiti, Tathmini na Huduma za Kompyuta, Joseph Mbowe baada ya uchunguzi kubaini kuwapo kwa dosari katika ukokotoaji wa alama za mitihani ya somo la Islamic Knowledge katika kompyuta.

Aidha, Wizara hiyo imeagiza Necta kukokotoa upya alama za mitihani ya wanafunzi wa kidato cha sita ya somo hilo waliofelishwa kwa bahati mbaya mwaka huu kutokana na dosari hiyo na tayari matokeo ya alama hizo yametolewa.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo na Ufundi, Philip Mulugo alisema Mei 28, mwaka huu, Wizara ilipokea malalamiko kutoka Baraza la Wakuu wa Shule za Kiislamu, dhidi ya matokeo ya wanafunzi wa kidato cha sita mwaka huu katika somo hilo.

Alisema baada ya Serikali kupokea malalamiko hayo iliunda tume ya watu tisa ikijumuisha wajumbe kutoka Wizara ya Elimu, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Wizara ya Elimu na Amali Zanzibar, Necta, Baraza la Elimu la Kiislamu, Baraza la Wakuu wa Shule za Kiislamu, Idara ya Usalama wa Taifa na Ofisi ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa.

Alisema kamati hiyo ilitakiwa kupitia orodha ya wasahihishaji wa somo hilo, kupitia maoni ya wasahihishaji, sampuli za mitihani za watahiniwa, kuhakiki uhamishaji wa alama kutoka mitihani kwenda kwenye kompyuta na kulinganisha mchakato wa usahihishaji na matokeo ya somo hilo kwa mwaka huu na miaka ya nyuma.

Mulugo alibainisha kuwa baada ya uchunguzi wa kamati hiyo ilibaini kuwa ukokotoaji wa alama za mitihani ya somo hilo ulikuwa na dosari kutokana na mfumo uliotumika kukokotolea kutofanyiwa marekebisho kulingana na mabadiliko ya sasa.

“Miaka ya nyuma somo hili lilikuwa linafanywa mitihani mitatu ambapo mfumo wa kompyuta ulikuwa unakokotoa na kugawanya alama kwa kutumia idadi hiyo ya mitihani mitatu, lakini mwaka huu tumebadilisha na mitihani ya somo hili ni miwili, lakini ukokotoaji uliotumika ni wa zamani wa kugawanya kwa mitihani mitatu,” alisema.

Alisema baada ya matokeo hayo, Serikali imeagiza Necta imchukulie hatua za kinidhamu Mbowe ambapo pia tayari wanafunzi waliofelishwa kutokana na dosari hiyo, alama zao za mitihani zimekokotolewa upya kwa mfumo wa sasa.

Sakata la kufeli kwa wanafunzi wa somo hilo mwaka huu, liliibua mjadala mkubwa ambapo Jumuiya na taasisi za Kiislamu zilifikia hatua ya kutaka Mkurugenzi Mtendaji wa Necta, Dk Ndalichako na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa wajiuzulu kutokana na uzembe uliotokea.