Tembo aingia ‘mjini’, ajeruhi watu watatu
- Imeandikwa tarehe 16 Septemba 2012
- By Thomas Dominick, Musoma
- Imesomwa mara: 507
WATU watatu akiwemo mwandishi wa habari wa kituo cha Radio cha Abood FM ya Morogoro, Mohammed Nyabange wamejeruhiwa na kukimbizwa Hospitali ya Mkoa wa Mara baada ya Tembo kuingia pembezoni mwa Manispaa ya Musoma mkoani hapo akitokea katika hifadhi ya Taifa ya Serengeti.
Tembo huyo aliuawa na askari wa wanyamapori kisha kuchukua meno, pembe na ngozi na nyama yake kuigawa kwa wananchi waliokuwepo eneo la tukio.
Akizungumza na gazeti hili, Nyabange alisema kuwa mnyama huyo aliingia maeneo ya Bweri pembezoni mwa manispaa hiyo usiku wa kuamkia jana na kuanza kuranda katika baadhi ya mitaa na kuzua hofu kubwa kwa wananchi na wakazi wa maeneo hayo.
Nyabange alimtaja aliyekuwa naye ni Rumegalila Jonath (35) mkazi wa kitongoji cha Mshande kijiji cha Nyabange Wilaya ya Butiama ambapo baada ya tukio hilo tulikimbizwa Hospitali ya Mkoa kwa matibabu zaidi.
Baada ya taarifa kuzagaa ndani ya Manispaa hiyo watu kutoka maeneo mbalimbali walifurika kumuona bila kujali hatari ambayo ingeweza kutokea huku wengine wakimrushia mawe na kupiga kelele ambapo mnyama huyo hapendi kelele.
Baadhi ya mashuhuda wa tukio hilo walisema kuwa tembo huyo alianza kumjeruhi mtu mmoja ambaye alikuwa na baiskeli alfajiri ya siku ya tukio lakini mtu huyo hakuweza kupatikana jina lake mara moja.


