21Mei2013

 

Uingereza yausifu uongozi wa Kikwete

SERIKALI ya Uingereza imeusifu uongozi wa Rais Jakaya Kikwete kwa kukuza demokrasia nchini, kutokana na uhuru unaovipa vyombo vya habari kuujuza umma mambo mbalimbali yakiwemo matumizi ya fedha za umma yanayofanywa na serikali yake.

Aidha, imesema uwepo wa mawasiliano yasiyo na vikwazo kati ya wanahabari na Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali nchini, umechangia kuufanya umma ufahamu kinachoendelea juu ya rasilimali zake na kuhoji wahusika pindi inapobaini matumizi mabaya ya rasilimali hizo.

Balozi wa Uingereza nchini, Duane Corner alizungumza hayo juzi wakati wa kufungua semina ya siku moja ya jinsi ya kuripoti masuala ya rushwa, yanayojitokeza katika ripoti za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa wanahabari na Mashirika yasiyo ya kiserikali (NGOs).

Alisema uhuru na uwazi huo usingekuwepo kama Rais na Serikali yake wangewanyima wanahabari uhuru wa kupata taarifa.

“Demokrasia ya Tanzania inakua siku hadi siku kutokana na imani ya Rais Jakaya Kikwete kwa vyombo vya habari inayowapa fursa ya kuufikishia umma taarifa kuhusu matumizi ya fedha za umma. Kama angezuia hata CAG asingeweza kueleza anayoyavumbua katika ukaguzi wake…”.

Kwa upande wake, CAG Ludovick Utouh alisema ofisi yake inatambua umuhimu wa vyombo vya habari nchini ndio maana inavipa taarifa zote muhimu ambazo umma unapaswa uzipate.