Madaktari wagawanyika
- Imeandikwa tarehe 19 Septemba 2012
- By Halima Mlacha
- Imesomwa mara: 1160
SIKU moja baada ya madaktari waliokuwa kwenye mafunzo kwa vitendo waliofukuzwa kazi kujitokeza na kuomba msamaha kwa kitendo chao cha kugoma na kusababisha madhara kwa wananchi, suala hilo limezua mgongano miongoni mwao baada ya wenzao kuibuka na kuwakana.
Hata hivyo, pamoja na Serikali kupongeza kitendo hicho cha madaktari hao kuomba msamaha ambacho ilikiita cha kizalendo, imesema bado suala lao lazima lishughulikiwe kisheria kwa kuzingatia nidhamu na taaluma ya udaktari.
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, mwakilishi wa madaktari waliokuwa kwenye mafunzo ya vitendo, Dk Frank Kagoro, alisema kundi la madaktari lililojitokeza na kuomba msamaha juzi kutokana na mgomo wa madaktari, halikuzingatia msimamo wa madaktari waliopo mafunzoni ambao walisimamishwa kazi.
“Kwa kweli hatuitambui kauli ya kuomba msamaha, kwa kuwa sisi kama interns tangu kuanza kwa mgogoro huu na kusimamishwa kazi takribani madaktari 360, tumekuwa tukishirikiana kwa kila kitu tunachokifanya lakini kwenye hili si wote tulioshirikishwa ni wachache tu ndio wamehusishwa na sisi tunashangaa,” alisema Dk Kagoro.
Alisema wanachofahamu kuhusu madaktari walioko kwenye mafunzo ya vitendo, ni kwamba bado suala lao liko mikononi mwa sheria na Baraza la Madaktari Tanzania (MCT) ndio linalochunguza ambapo upo utaratibu wa kila daktari aliyesimamishwa kuhojiwa na Baraza hilo.
“Tunapenda ieleweke kuwa suala la madai ya madaktari si tukio, bali mchakato utakaoendelea kwa vizazi vya sasa na vijavyo…kuna kikundi kinachotumiwa kuomba msamaha kwa lengo la kudhalilisha taaluma na kurudisha nyuma jitihada za kuboresha hali ya afya nchini na maslahi ya umma,” alisisitiza.
Alisema mpaka sasa Kamati ya Jumuiya ya Madaktari Tanzania haijui kilichosababisha madaktari hao kuomba msamaha, kwa kuwa suala hilo liko wazi kuwa lipo bado kwenye mikono ya sheria ambapo pia hadi sasa hakuna dai hata moja lililoshughulikiwa na Serikali.
“Hata hivyo, nashangaa wameomba msamaha wa kitu gani kwa sababu inafahamika duniani kote kuwa madaktari wa vitendo huwa wako chini ya madaktari bingwa, hivyo jambo lolote likiharibika hulaumiwa daktari bingwa, hata kwenye huu mgomo lawama si za interns sasa sijui wenzetu walikuwa wanafikiria nini?” Alihoji Makamu Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo, Dk Godbless Charles.
Aidha, Dk Charles aliwaasa madaktari wote waliosimamishwa katika kipindi hiki kuepuka kutumiwa na kikundi cha wanaowatumia kwa maslahi ya kufurahisha watawala.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Seif Suleiman Rashid, aliwapongeza madaktari hao kwa kitendo chao cha kuomba msamaha lakini aliwashauri kuuwasilisha rasmi msamaha huo kwa maandishi serikalini.
Pia alibainisha wazi kuwa pamoja na msamaha huo, bado Serikali haiwezi kufanya jambo lolote kwa kuwa suala hilo kwa sasa limefikia katika hatua ya kisheria zaidi.
“Suala hili linatakiwa kushughulikiwa kisheria kwa kuangalia nidhamu na taaluma ya udaktari na ndiyo maana tunasisitiza kuwa lazima utaratibu wa MCT ufuatwe kwa interns kuhojiwa ingawa nawasifu na kuwapongeza kuwa walichokifanya ni uzalendo,” alisema Dk Rashid.
Rais wa MCT , Dk Donan Mbando alisema hawezi kuzungumzia suala la msamaha kwa sasa, kwa kuwa suala hilo litaamuliwa na Baraza. “Sisi hatushughuliki na kundi la watu bali mtu mmoja, baada ya Baraza kumaliza kazi yake, tutajua nani anapewa adhabu au kusamehewa,” alisema Dk Mbando.
Askofu amwomba JK
Naye Kareny Masasy anaripoti kutoka Shinyanga, kwamba Askofu Edson Mwombeki amemwomba Rais Kikwete apokee maombi ya msamaha ya madaktari hao.
Akizungumza na waandishi wa habari katika Kanisa la Tanzania Evangelism Field (TEF) mjini humo jana, alimuomba Rais ayapokee huku akifananisha madaktari hao na wana wapotevu waliokuwa wamepotea kwa baba yao na walipokumbuka walirudi kuomba msamaha.
“Akiwa Rais wa nchi anahitaji kuwasamehe, maana hata sisi viongozi wa dini katika maombi yetu kwa nchi, suala la madaktari ambalo halikutufurahisha tuliliombea mara kwa mara hivyo nimejisikia furaha kuona wanajitokeza na kuomba msamaha,” alisema Mwombeki.
Mwombeki alisema msamaha ulioombwa na madaktari kwa Watanzania na Rais unatakiwa ukubaliwe kwa kuwa wameona makosa yaliyofanyika na kuhisi wanahitaji kusamehewa kama maandiko ya Mungu yanavyosema.
Aliwasihi wafanye kazi bila kuangalia maslahi bali ubinadamu na kulipenda Taifa na watu wanaohudumia na kumtanguliza Mungu kwa kila jambo.
Mgomo
Madaktari hao katika mgomo wao walikuwa wakidai wanaoanza kazi walipwe mshahara wa Sh milioni 3.5 kutoka Sh 957,700 na posho ya kuitwa kazini baada ya saa za kazi kuwa asilimia 10 ya mshahara, posho ya mazingira hatarishi kuwa asilimia 30 ya mshahara na madaktari kupewa nyumba au posho ya nyumba sawa na asilimia 30 ya mshahara.
Pia walitaka posho ya mazingira magumu ya asilimia 40 ya mshahara, posho ya usafiri ya asilimia 10 ya mshahara, au kukopeshwa magari; kupewa kadi za kijani za Bima ya Afya; kurekebisha malipo ya posho ya kuchunguza maiti na kuchukua hatua dhidi ya viongozi wakuu wa wizara.
Madai mengine ni kupewa chanjo ya Hepatitis B; kuboresha huduma zinazotolewa kwa wananchi; kurudishwa kazini kwa madaktari walio mafunzoni waliopangiwa vituo vingine na viongozi waache kulazimisha rufaa ya matibabu nje ya nchi.
Hatua za Serikali
Serikali baada ya kutafakari, iliamua kuunda Kamati chini ya uenyekiti wa Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma ambayo ilifanya mazungumzo na wawakilishi wa madaktari kuhusu madai 12 yaliyowasilishwa serikalini.
Baada ya mazungumzo hayo, Serikali ilikubali kuongeza kiwango cha posho ya kuitwa kazini baada ya saa za kazi na kuanza kulipa rasmi Februari mwaka huu; kutenga fedha katika bajeti ya mwaka 2012/13 za chanjo ya Hepatitis B na kutoa kadi ya kijani ya Bima ya Afya kwa madaktari wote.
Pia Serikali ilikubali madaktari wakopeshwe fedha kwa ajili ya ununuzi wa magari kwa kuzingatia taratibu zilizopo za utumishi wa umma; kuboresha huduma za afya nchini kwa kuongeza bajeti ya sekta ya afya ili kuboresha miundombinu, ununuzi wa dawa, vifaa, vifaa tiba na vitendanishi na kuboresha maslahi ya watumishi.
Katika posho, Serikali lilikubali kuongeza posho ya kuchunguza maiti kutoka Sh 10,000 hadi Sh 100,000 na kurudishwa Muhimbili kwa madaktari walio mafunzoni waliokuwa wamerudishwa wizarani katika mgomo wa awamu ya kwanza wa Februari.
Hata hivyo pamoja na jitihada hizo za Serikali, ikiwa ni pamoja na viongozi wakuu wa wizara, kuondolewa kazini, madaktari hawakuridhia na waligoma tena mara ya tatu kuanzia Juni 23.
Kutokana na mgomo huo, Rais Kikwete aliagiza madaktari ambao hawakubaliani na mshahara unaolipwa na Serikali wawe huru kuacha kazi kwa hiari yao, kwa sababu Serikali haina uwezo wa kulipa mshahara wanaotaka.



