25Mei2013

 

Helikopta kutumika kutimua wafugaji

HELIKOPTA nne zinatarajiwa kutumika kuongeza kasi ya kuhamisha mifugo na kusitisha kazi ya kilimo katika maeneo tengefu
ya Bonde la Kilombero.

 

Hayo yalisema na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Joel Bendera juzi, kwa nyakati tofauti mjini Mahenge na Ifaraka wakati wa vikao maalumu vya baraza la Madiwani vilivyoitishwa kujadili na kupata maelekezo ya Mkoa yatokanayo na taarifa ya Ukaguzi iliyotolewa na CAG.

Muda wa hiari wa kuondoka katika eneo hilo na kuacha shughuli za kilimo na ufugaji ulikuwa Septemba 8, mwaka huu.

Mkuu huyo wa mkoa alisema, hadi juzi kiasi cha malori zaidi ya 40 yamesafirisha shehena ya ng’ombe kutoka Bonde la Kilombero kwenda sehemu walikotokea ikiwemo Makuyuni mkoani Arusha.

Hata hivyo alisema, ili kufanikisha jukumu hilo, Serikali kuu imetoa helikopta nne zitakazotumika kwa kazi hiyo maalumu kwa lengo la kuhakikisha makundi ya ng’ombe na wakulima waliopo ndani ya hifadhi ya bonde la Kilombero na maeneo tengefu wameondoka wote.

Kwa mujibu wa Mkuu wa Mkoa, mifugo mingi iliyokuwemo ndani ya Bonde hilo imetoka maeneo ya Ihefu, Mkoa wa Mbeya na mingine ya Ziwa Magharibi na kutokana na ulegevu wa usimamizi wa sheria za vijiji na viongozi wake, mifugo hiyo ilipenyezwa katika Wilaya ya Kilombero na Ulanga.

“Wilaya ya Kilombero na Ulanga hakukuwa na ng’ombe, ni eneo la Kilimo, lakini hivi sasa kuna rundo la ng’ombe zaidi ya 300,000 kwa upande mmoja wa Wilaya, tumepewa jukumu na Rais kwa Wilaya hizi mbili ziwe za uzalishaji wakuu wa mpunga tani milioni 1.5 kwa mwaka,“ alisema mkuu huyo wa mkoa.

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya hiyo, Furaha Lilongeli, alisema baraza hilo lenye madiwani 42 wameamua kusimama kidete kuhakikisha operesheni hiyo inatekelezwa na kusimamiwa kwa kufuata sheria zote bila kuwaonea wakulima na wafugaji ambao wanatakiwa kuondoka maeneo tengefu.

Serikali kuu kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira) iliwataka watu wote waliovamia maeneo tengefu na mabonde yote nchini kuondoka wenyewe kabla ya kuondolewa kwa nguvu na kwa Bonde la Kilombero walitakiwa wawe wameondoka kwa hiari yao ilipofika Septemba 8, mwaka huu.