Shehe Ponda bado alia na Mufti
- Imeandikwa tarehe 22 Septemba 2012
- By Oscar Job
- Imesomwa mara: 2223
KATIBU Mkuu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu nchini, Shehe Issa Ponda, jana alirejea kauli zake za kufanya maandamano ya kumng’oa madarakani Shehe Mkuu wa Tanzania, Mufti Issa bin Shaaban Simba na Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani la Tanzania (NECTA), Dk Joyce Ndalichako.
Pamoja na kauli hizo pia alitaka ubalozi wa Marekani nchini kufungwa.
Akihutubia katika maandamano ya kulaani filamu inayodaiwa kumdhalilisha Mtume Muhammad (S.A.W) uliofanyika katika kiwanja cha Kidongo Chekundu Shehe Issa Ponda, alidai kuwa Marekani imekuwa ikifanya vitendo vya kidhalimu dhidi ya waumini wa dini ya Kiislamu.
Akisoma tamko katika Mkutano huo ulioanza saa 7 mchana hadi saa 11 jioni, Shehe Ponda, amesema Waislamu nchini wanalaani watu walioitengeneza filamu hiyo huku akiitaka Serikali kupiga marufuku mitandao yote kuendelea kuionesha filamu hiyo.
“Pamoja na maneno yote yanayoongelewa, lengo la kumng’oa Mufti lipo pale pale, Bakwata pia, tunataka haki kwa Waislamu, siku zao zinahesabika hakuna kulala mpaka kieleweke,” alisema Shehe Ponda.
Hata hivyo, tamko hilo linakuja siku tatu baada ya Baraza Kuu la Waislamu Tanzania kupitia kwa Kiongozi wake Mufti Issa bin Shaaban Simba kutoa tamko lao kupinga utengenezwaji wa filamu hiyo.



