25Mei2013

 

Familia ya Nyerere yaunganishwa kesi ya mauaji

NDUGU wa Baba wa Taifa, Makongoro Joseph Nyerere amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam akikabiliwa na mashitaka ya mauaji.

Nyerere ambaye ni mtoto wa mdogo wake Mwalimu Julius Nyerere, alifikishwa mahakamani hapo jana na kuunganishwa katika kesi ya mauaji inayomkabili mfanyabiashara Marijani Abubakari ‘Papaa Msofe’.

Wakili wa Serikali Charles Anindo alidai mbele ya Hakimu Mkazi Agness Mchome, kuwa Novemba 6 mwaka juzi katika eneo la Magomeni, Nyerere alimuua mfanyabiashara Onesphory Kitoli.

Hata hivyo mshitakiwa hakutakiwa kujibu mashitaka kwa kuwa, mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi za mauaji isipokuwa Mahakama Kuu.

Nyerere ameunganishwa na Papaa Msofe ambaye alifikishwa mahakamani hapo Agosti mwaka jana na kusomewa mashitaka hayo.

Washitakiwa wataendelea kusota rumande hadi kesi hiyo itakapokwisha kwa kuwa kisheria shitaka linalowakabili halina dhamana.

Kesi hiyo imefunguliwa mahakamani hapo katika hatua za awali ambapo upelelezi utakapokamilika itahamishiwa katika Mahakama Kuu kwa ajili ya kuanza kusikilizwa.