Wanaume Handeni wakwepa kutumia choo na watoto
- Imeandikwa tarehe 04 Machi 2013
- By Bantulaki Bilango, Morogoro
- Imesomwa mara: 512
WAZAZI wa kiume wametajwa kuchangia usugu wa kipindupindu katika Wilaya ya Handeni mkoa wa Tanga, kutokana na kuendekeza imani kwamba, hawapaswi kutumia choo kimoja na watoto wao wa kike na wakwe zao.
Utafiti uliofanywa na wahadhiri wa Chuo Kikuu cha Ardhi, mbali na kubaini imani hiyo, pia ulibaini kwamba wenyeji wengi katika Wilaya hiyo, bado wanaamini kwamba ugonjwa wa kipindupindu kila mmoja anaweza kuupata, kwa kuwa unaambukizwa kutokana na matakwa ya Mwenyezi Mungu.
Akiwasilisha utafiti huo kwenye warsha ya siku mbili iliyoandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, Idara ya Uratibu wa Maafa, Dk Joseph Mayunga wa Chuo cha Ardhi, alisema mwishoni mwa wiki kuwa wenyeji wengi wa Handeni, hawatumii choo na badala yake wanajisaidia vichakani.
Alisema wenyeji wengi wanaume, wanaamini kuwa si sahihi kinyesi chao kuunganishwa pamoja na cha watoto wao wa kike na wakwe zao.
Kutokana na imani hiyo, Dk Mayunga alisema njia wanayoitumia kuepuka hilo, ni kila mmoja kuchimba shimo lake kichakani na kwenda kujisaidia, jambo ambalo linazidisha milipuko ya ugonjwa huo.
Katika utafiti huo, kazi waliyopewa na Ofisi ya Waziri Mkuu, Kitengo cha Maafa katika kutafuta suluhisho la mawasiliano ya haraka kabla, wakati na baada ya matukio ya maafa yakiwemo ya ugonjwa huo, ilibainika kwamba Wilaya ya Handeni imekuwa ikikabiliwa na kipindupindu katika kipindi chote cha mwaka.
“Hii inatokana na imani potofu kwa kuwa jamii ina uelewa mdogo juu ya maambukizo ya ugonjwa huo ikiwemo kuamini kwamba kila mmoja anaweza kupata ugonjwa huo kutoka kwa Mungu,” alisema.
Utafiti huo ambao ulikuwa ukipitiwa na wajumbe wa warsha hiyo kabla ya kutumika kwa walengwa, ulibainisha kwamba zaidi ya asilimia 40 ya waliohojiwa, walisema kipindupindu kimekuwa kikitokana na utamaduni duni wa kuhifadhi vinyesi vya binadamu.
Mmoja wa watafiti hao, Fredrick Salukele, alisema ugonjwa huo umeenea katika maeneo yote yakiwemo ya vijijini na mjini katika wilaya hiyo, kutokana na imani hiyo na kupendekeza ichukuliwe hatua ya haraka kukabiliana na hali hiyo.
Katika kukabiliana na tatizo hilo, watafiti wamependekeza njia mbalimbali zitumike kutoa elimu kwa walengwa zikiwemo za matangazo katika televisheni, redio, magazeti, mabango, vipeperushi na ngoma za asili.
Mbali na Wilaya ya Handeni, pia utafiti huo ulifanywa katika wilaya nyingine tano ukihusisha matukio makubwa matatu; ukame, mafuriko na milipuko ya ugonjwa wa kipindupindu. Kati ya wilaya hizo, nne zilikuwa za Tanzania Bara na mbili za Zanzibar.
Katika visiwa vya Zanzibar, utafiti ulifanyika katika Wilaya ya Magharibi Unguja juu ya mafuriko na Wilaya ya Micheweni juu ya ukame. Kwa upande wa Tanzania Bara, utafiti ulifanyika katika wilaya za Longido, Arusha (ukame), Kilosa, Morogoro (mafuriko) na Kindondoni, Dar es Salaam (mafuriko).
Akifunga warsha hiyo, Mkurugenzi wa Idara hiyo ya Uratibu wa Maafa, Ofisi ya Waziri Mkuu, Silvester Rioba, aliitaka jamii kubadilika ili kukabiliana na majanga huku akitaka viongozi wa jadi kutumika kuelimisha jamii husika.



