18Mei2013

 

Wasifu udhibiti wa redio

WANANCHI jijini Dar es Salaam, wameipongeza Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), kwa uamuzi wake wa kufungia redio mbili za FM zilizokiuka maadili.

Wiki iliyopita Mamlaka hiyo ilifungia kwa miezi sita redio mbili za dini ambazo ni Iman FM iliyopo Morogoro na Kwa Neema FM iliyopo Mwanza.

Redio hizo zilifungiwa baada ya kurusha matangazo ambayo kwa mujibu wa TCRA, yangeleta uchochezi na uvunjifu wa amani nchini.

Redio ya Iman FM ilikutwa na hatia ya kurusha matangazo wakati wa Sensa ya Watu na Makazi mwaka jana, kuhamasisha waumini wa Kiislamu wagome kuhesabiwa.

Kwa Neema FM ilikutwa na hatia ya kushiriki kuchochea vurugu za kidini, zilizotokea hivi karibuni mkoani Geita, ambapo baadhi ya Waislamu na Wakristo, walitofautiana juu ya nani anastahili kuchinja.

Mamlaka hiyo pia imepiga marufuku kipindi cha Jicho la Ng’ombe, ambacho kimekuwa kikirushwa ndani ya kipindi cha asubuhi cha Power Breakfast cha Redio ya Clouds.

“Huu ni mwanzo wa safari yetu ndefu ya kuhakikisha redio hizi za FM zinafuata maadili na taaluma, kwa kuwa kwa sasa redio nyingi zimekuwa zikipindisha maadili ili kuvutia wasikilizaji,” alisema mkazi wa Mbagala, Rajabu Mkude.

Mkude pia aliitaka TCRA kuwa makini, kutokana na kuchipukia kwa redio ambazo baadhi yake zimeanza kupoteza mwelekeo.
Mkazi mwingine wa Dar es Salaam, Joyce Mlindwa aliitaka Serikali kuandaa muswada wa sheria na kuuwasilisha bungeni, utakaoeleza ni sifa zipi hasa zinafaa kwa mtangazaji.

“Siku hizi watangazaji wengi wanaajiriwa kwa sababu tu wana sauti nzuri, wengi wao hawajaenda shule na matokeo yake hawana
uelewa wa kutosha kuhusu maadili ya kazi zao,” alisema.

Shehe Khamis Muhammed kutoka Ilala Sharif Shamba, alisema wamiliki wa redio hizo wanatakiwa kutambua kuwa Tanzania kama nchi, inayo sheria zake zinazodhibiti sekta ya utangazaji na ni wajibu wao kuhakikisha sheria hizo zinafuatwa.

“Redio hizi hazitakiwi kujiendesha kama taasisi za wanaharakati hata siku moja, uanaharakati hauwezi kwenda pamoja na taaluma,” alisisitiza.

TCRA pamoja na kuzifungia redio hizo mbili, pia imeagiza redio zote tatu kila moja kulipa faini ya Sh milioni tano. Aidha, Mamlaka hiyo ilitoa onyo kwa watangazaji wote nchini, ambao watakwenda kinyume na Sheria na Kanuni za utangazaji.

Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili ya Utangazaji wa TCRA, Walter Bgoya alisema redio zote Kwa Neema FM na Iman FM zimetakiwa kuandika zenyewe kuwa hazitorudia tena kosa walilofanya.

Alihadharisha kuwa wadhibiti wa TCRA hawatosita kunyang’anya leseni redio yoyote itakayorudia makosa hayo.