Tanesco yadai hakuna ‘mgawo’ wa umeme
- Imeandikwa tarehe 05 Machi 2013
- By Mwandishi Wetu
- Imesomwa mara: 465
PAMOJA na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) , kutangaza kuwa hakuna mgawo wa umeme, lakini wakati wa mahitaji makubwa ya umeme hasa usiku, limekuwa likilazimika kuendesha mgawo mdogo.
Akizungumza jana Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Tanesco, Felchesmi Mramba, alisema kuwa pamoja na kuzalisha umeme kwa kutegemea mitambo ya dharura, hakuna mabadiliko yoyote yaliyotokea yatakayofanya kuwapo kwa mgawo wa umeme.
“Hakuna jambo lolote jipya lililotokea, bado hali ya maji ni kama ilivyokuwa mwaka jana, bado tuko kwenye hali ya dharura, lakini umeme umeendelea kupatikana na ndivyo hali itakavyoendelea kuwa. Uwezo wa kuzalisha umeme upo, kinachotakiwa ni fedha ya kununulia mafuta,” alisema.
Hata hivyo, alikiri kuwa mahitaji ya umeme kwa nchi nzima ni wastani wa megawati 750 kwa siku na kuwa nyakati za matumizi makubwa, ambazo ni kuanzia saa 12 jioni mpaka saa tano usiku, hufikia megawati 850.
Kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa na Mramba jana, wakati uwezo wa kuzalisha umeme wa maji ni kati ya megawati 120 hadi 130, umeme unaozalishwa na gesi kutoka Songosongo ni megawati 330 na umeme wa mafuta ni megawati 365.
Kutokana na takwimu hizo, inaonesha kuwa katika hali ya kawaida Tanesco huwa na uwezo wa kuzalisha megawati 825 na hivyo wakati wa usiku, kuanzia saa 12 jioni mpaka saa 5 usiku, hukabiliwa na upungufu wa megawati 25 kwa kuwa mahitaji hufikia megawati 850.


