20Mei2013

 

Salma: Wazazi mnachangia watoto kuzembea masomo

ILIKUWA patashika nguo kuchanika.

Akinamama walilazimika kukimbia kila upande kurejea majumbani mwao huku wengine wakificha nyuso zao na kujitenga mbali na mkutano wa hadhara uliokuwa unaoendelea. Akinamama hao, huku wakiongozwa na baadhi ya wanaume ambao baadaye ilifahamika kuwa ni waume zao, walikuwa wakikimbia aibu.

Hii ilikuja baada ya watoto wao ambao hawakwenda shule kutakiwa kwenda mbele ya mkutano huo huku kila mmoja akiwa amemshika mzazi wake mkono! Sakata hilo, lilijitokeza juzi mkoani Lindi wakati Mke wa Rais ambaye pia Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Lindi mjini, Salma Kikwete, alipokuwa akihutubia mjini humo.

Akiwa Lindi, Mama Salma alitembelea kata zote 18 za halmashauri ya Manispaa ya Lindi, ikiwa ni ziara yake ya kushukuru wanachama wa CCM kumchagua katika nafasi hiyo, lakini pia kukagua na kuimarisha uhai wa chama. Takribani katika mikutano yake yote ya hadhara, Mama Salma ambaye kitaaluma ni mwalimu alionesha kusikitishwa na idadi kubwa ya watoto wenye umri wa kwenda shule wanaozagaa mitaani.

Katika mikutano yake minne, alilazimika kutuma askari kuwakusanya watoto hao na kupelekwa mbele yake. “Nyie nawauliza mnasoma?” alihoji katika mkutano mmoja ambapo watoto takribani 30 wenye umri wa kwenda shule walikusanywa mbele yake katika wakati huo ambao ulikuwa ni wa shule.

Walijibu kwamba wanasoma lakini hawakwenda shule siku hiyo bila sababu, jambo ambalo lilimpandisha hasira mama huyo na kuwataka kila mmoja ampeleke mzazi wake mbele yake ili wajieleze kwa nini hakumshurutisha kwenda shule.

Huku wakati mwingine akilazimika kuongea lugha ya Kimalaba, maarufu kama Machinga akisisitiza mtoto anayemuona mzazi wake pale mkutanoni amshike mkono, ndipo na kumleta jukwaani, ndipo ukatokea mshikemshike huo wa wazazi kutimua mbio wakikimbia aibu.

“Hivi kwa nini watoto wengi nawaona hapa leo Jumatatu wakati wanatakiwa wawe shuleni? Haya naomba watoto wote waliopo hapa waje jukwaani,” alisema Mama Salma katika mkutano mwingine ambapo safari hii takribani watoto 40 walipanda jukwaani. Baada ya hapo akaita wazazi wao wapande jukwaani lakini hakuna aliyejitokeza.

Baada ya kimya, Mama Salma Kikwete akawageukia watoto hao: “Kwa nini hamjaenda shule? Kila mtoto aliyepo hapa akaorodheshe jina lake kwa msaidizi wangu halafu akamshike mkono mzazi wake aje naye hapa mbele.” Kama ilivyotokea awali, mbio zikaanza tena katika mkutano huo mwingine.

Pamoja na wazazi hao kukimbia, mama Salma aliendelea kuwahoji watoto hao na kuwashauri wapende elimu kwa kuwa ndio mkombozi na daraja la mafanikio kwao hapo baadaye. Aliwageukia wazazi akiwashauri kujua kwamba wao ndio nguzo kuu ya mafanikio ya elimu kwa watoto wao.

“Jamani narudia tena kusema hili, kama wazazi tusikwepe jukumu letu. Hivi kweli tunawaachia watoto wetu na kuwaangalia tu pale wanapogoma kwenda shule? Nyie watoto nimewaita hapa mbele kuwahimiza muende shule kwa faida yenu,” alisisitiza.

Mke wa Rais anasema inasikitisha kuona wazazi hawatoi ushirikiano na kusaidia walimu na Serikali katika kusimamia watoto waende shule, jambo ambalo limesababisha mkoa wa Lindi kuwa miongoni mwa mikoa inayoshika nafasi ya mwisho kielimu.

“Inauma lakini ndio ukweli wenyewe, Lindi inashika nafasi ya mwisho kielimu hata mwaka huu takribani shule 10, tena zote za Lindi zimeshika mkia. Haya (ya watoto kutokwenda shule) ndio yanayosababisha. Hii si sawa, lazima tusimamie watoto wetu wasome, hawa ndio tegemeo la kesho,” anasema.

Katika kuonesha kuwa tatizo hilo mkoani hapo ni kubwa mkazi wa kijiji cha Narunyu, Hamisi Mohammed, alielezea kusikitishwa kwake na uduni wa elimu mkoani Lindi, hali iliyosababisha moja ya shule ya msingi (hakuitaja) ifaulishe mwanafunzi mmoja pekee katika mtihani wa darasa la nne. “Mheshimiwa Mama Salma, hali ya elimu hapa mkoani kwetu hairidhishi sijui utatusaidiaje.

Hivi inakuwaje wanafunzi wote wa darasa la nne wafeli mtihani wa darasa la nne, na afaulu mwanafunzi mmoja tu?” akahoji Mohammed. Akijibu swali hilo, Mama Salma alikiri kuwa bado kuna changamoto nyingi katika sekta ya elimu, ikiwemo uhaba wa walimu na upungufu wa vifaa lakini pia alisema changamoto nyingine zinapaswa kutatuliwa na wananchi wenyewe hasa zile ambazo wana uwezo nazo.

Anasema wazazi na walezi wengi hawana utamaduni wa kufuatilia maendeleo ya watoto wao shuleni, wala kushiriki katika maendeleo yeyote yanayohusu sekta ya elimu, hali inayowaongezea walimu na Serikali mzigo mkubwa katika kuhakikisha elimu bora inapatikana. Anabainisha kuwa mzazi yeyote anatakiwa angalau kwa mara tatu au mbili kwa mwezi kwenda shuleni na kuulizia maendeleo na mwenendo mzima wa kimaadili wa mtoto wake.

“Tusiwaachie walimu na Serikali pekee yao, hili ni jukumu letu sote, sisi ndio Serikali tukumbuke hili, sio mtoto ukimwambia aende shule akikataa basi na wewe ubaki tu kusema ah amekataa bwana, huyu ni mwanao onesha unajali,” anasisitiza. Anasema ili sekta ya elimu iweze kuendelea ni lazima kuwepo ushirikiano baina ya wazazi na walimu na ndio maana katika kila shule kuna kamati za shule ambazo wajumbe wake ni wazazi na walimu.

Hata hivyo, Mama Salma anakanusha kuwa mkoani huo bado ni duni kimaendeleo. Anasema kwa kiasi kikubwa serikali imefanikiwa kuboresha mazingira ya elimu ambapo kwa sasa kuna shule nyingi za msingi na sekondari ikilinganishwa na miaka ya nyuma.

“Mimi jamani ni mzaliwa wa hapahapa, Lindi mnayoiona sasa si Lindi ya zamani, zamani kulikuwa na shule mbili mkoa mzima za sekondari, ya Mkonge na Lindi mjini. Nafasi za kujiunga kwenye shule hizo wakati mwingine zilikuwa wanafunzi 16 tu mkoa mzima,” anasema.

Kwa sasa hali imebadilika, shule zimekuwa nyingi hasa za kata na wanafunzi wengi wanapata fursa ya kuendelea na elimu ya sekondari na kinachotakiwa ni usimamizi thabiti kutoka pande zote; wazazi, walimu na serikali kwa kuwa kitu kimoja, anasema. Pamoja na hayo mama huyo anawatoa hofu walimu wanaopangiwa maeneo ya vijijini akiwataka wasiyakimbie na kujitolea kwa faida ya nchi yao kwa kuwa hata hivyo, huko ndiko kwenye riziki yao.

Anajitolea mfano yeye mwenyewe alivyoweza kumudu alipopangiwa katika kijiji cha Chikonji kufundisha na kufanikiwa kimaisha. “Mimi eneo langu la kwanza kupangiwa kufanya kazi ni Shule ya Msingi Chikonji, wakati huo si Chikonji hii sasa, pori lilikuwa pori kweli ukizubaa unaliwa na simba, tena kuja huku nilikuja kwa trekta kwa kuwa barabara ilikuwa mbaya, lakini nawaambieni mume wangu (ambaye sasa ni Rais) nilimpatia hukuhuku porini,” anasema.

Naye Meya wa Manispaa ya Lindi, Frank Magali anawataka wananchi kusaidia walimu katika kujenga maadili na malezi bora kwa watoto na si kufumbia macho vitendo viovu dhidi ya walimu vinavyofanywa na watoto hao ikiwemo walimu kupigwa. Anatolea mfano tukio lililotokea wilayani hapo hivi karibuni ambapo mwanafunzi alimpiga mwalimu na kumtoa meno lakini hakuna hata mzazi mmoja aliyechukua hatua ya kukemea au angalau kufuatilia chanzo cha ugomvi huo.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Lindi Mjini, Dk Nassoro Ally, anasema wilaya hiyo inatarajia kupata walimu 200 ambao wakiwasili mkoani hapo watahitaji nyumba za kuishi na kuwasihi wananchi wasaidie katika ujenzi wa nyumba hizo.

Aidha anawataka wazazi kushirikiana na serikali za mitaa pale watoto wao wanapokuwa watukutu na kukataa kwenda shule huku akizisititiza kwamba serikali zote za mitaa nchini na za vijiji zinatakiwa kufuatilia kwa makini uhudhuriaji wa watoto mashuleni.

Akiwa wilayani hapo mama Salma alitembelea kata ya Chikonji, Mtanda, Tandangongoro, Ng’apa, Msinjahili, Mitandi, Mbanja, Rasibura, Mwenge, Jamhuri, Makonde, Ndoro, Mitopeni, Wailes na Mikumbi.

y>