22Mei2013

 

Yanga yatulizwa Mbeya, Simba moto mkubwa

SIMBA imeanza kwa kishindo Ligi Kuu Tanzania Bara baada ya kuifunga African Lyon mabao 3-0 katika mchezo wa fungua dimba ya Ligi Kuu Tanzania Bara kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Simba ambao ni mabingwa watetezi wa ligi hiyo walienda mapumziko wakiwa mbele kwa mabao 2-0 hivyo kuwapa furaha mashabiki wao ambao Jumanne pia timu yao ilitwaa Ngao ya Jamii kwa kuifunga Azam mabao 3-2.

Bao la kwanza la Simba jana lilifungwa dakika ya 33 mfungaji akiwa mshambuliaji wa kimataifa wa Uganda, Emmanueli Okwi aliyefunga kwa shuti kali tokea upande wa kulia wa uwanja.

Baada ya kuingia kwa bao hilo, Simba inayodhaminiwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kupitia Bia ya Kilimanjaro Premium Lager, iliendelea kuliandamana lango kwa pasi nzuri kupitia kwa washambuliaji wake Haruna Moshi, Mwinyi Kazimoto na Amri Kiemba.

African Lyon walipata penalti dakika 35 baada ya kiungo Mwinyi Kazimoto kuunawa mpira kwenye eneo la penalti na mwamuzi Oden Mbaga kuamuru penalti hiyo kupigwa kuelekea lango la Simba.

Mshambuliaji mkongwe wa timu hiyo Sunday Bakari alikosa penalti hiyo baada ya kupanguliwa na mlinda mlango wa Simba, Juma Kaseja na kisha kuokolewa na mabeki wa Simba na kusababisha shambulizi kali la kushtukiza.

Katika shambulizi hilo, mshambuliaji Mrisho Ngassa alikimbia na mpira na kumpa pasi Nassoro Masoud ‘Cholo’ aliyefunga bao la pili kwa Simba kwenye dakika ya 36.

African Lyon iliwapumzisha Johanes Kajuna, Sunday Hinju na Idd Mbaga na kuwaingiza Adam Kingwande, Hood Mayanja. Mabadiliko hayo hayakuonekana kuisaidia sana African Lyon kwani waliruhusu bao la tatu lililofungwa Daniel Akuffo kwa njia penalti baada ya mshambuliaji Okwi kuangushwa eneo la penalti.

Simba nayo ilifanya mabadiliko kwa kuwatoa Haruna Moshi na Daniel Akuffo na kuwaingiza Salim Kinje na Ramadhani Chombo ‘Redondo’ mabadiliko ambayo hakubadili sura ya mchezo.

Kwenye mchezo wa jana Simba haikuwachezesha mabeki wake wa kati, Komanbil Keita na Paschal Ochieng na badala yake ikawachezesha Shomari Kapombe na Juma Nyosso walioonekana kuelewana sana kwenye nafasi hiyo.

SIMBA: Juma Kaseja, Nassor Masoud, Amiri Maftah, Shomari Kapombe, Juma Nyoso, Mwinyi Kazimoto, Amri Kiemba, Haruna Moshi/Salim Kinje, Daniel Akuffo/Ramadhani Chombo, Mrisho Ngassa, Emmanuel Okwi.

African Lyon:Abdul Seif, Johanes Kajuna/Kingwande, Hamadi Manzi, Sunday Bakari, Benedictor Mwamlangala, Sunday Hinju/Hood Mayanja, Obina Salamusa, Semmy Kessy, Idd Mbaga/Mohamedi Samatta, Jacob Masawe, Yusuf Mlipili.

Ligi hiyo inayoshirikisha timu 14 ilianza jana katika viwanja saba, ambapo licha ya mechi ya Simba dhidi ya Lyon, nyingine ilikuwa kati ya Yanga na Prisons uliofanyika Uwanja wa Sokoine Mbeya.

Polisi Morogoro ilicheza na Mtibwa Sugar (Jamhuri, Morogoro), Mgambo JKT vs Coastal Union (Mkwakwani, Tanga), JKT Ruvu vs Ruvu Shooting (Azam Complex, Dar es Salaam), Kagera Sugar vs Azam (Kaitaba, Bukoba) na Toto Africans vs Oljoro JKT (Kirumba, Mwanza).

Mwandishi Wetu Cosmas Mlekani anaripoti kutoka Mbeya kuwa Yanga ambayo kama Simba ilifanya usajili wake kwa mbwembwe kwa kuchukua wachezaji kutoka nje ya Tanzania, jana ilijikuta ikishindwa kutamba kwenye Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya baada ya kutoka 0-0 na Prisons.

Ulikuwa mchezo wa vuta nikuvute, ambapo washambuliaji wa Yanga inayodhaminiwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kupitia Bia ya Kilimanjaro Premium Lager, wakiongozwa na Didier Kavumbangu, Said Bahanunzi, Hamisi Kiiza na Stephano Mwasika walijaribu mara kadhaa kuingia ndani ya eneo la hatari, lakini umaliziaji haukuwa mzuri.

Mwasika alipata nafasi nzuri ya kufunga dakika ya nane, lakini alipiga shuti lililopaa juu kidogo ya lango. Nao washambuliaji wa Prisons iliyorejea tena ligi hiyo msimu huu wakiongozwa na Elias Maguli, Sino Agostino na Peter Michael nao umaliziaji ulikuwa butu kwa kushindwa kulenga lango au kupiga michomo dhaifu iliyodakwa na kipa Ali Mustapha ‘Barthez’.

Kiungo Mbuyu Twite ambaye usajili wake ulitawala vyombo vya habari safari hii, nusura aipatie Yanga bao dakika ya 13, lakini shuti lake halikulenga lango, dakika chache baadaye Kiiza alipiga mpira uliombabatiza kipa na kuwa kona butu.

Kipa wa Prisons, David Abdallah jana alikuwa kikwazo kikubwa kwa Yanga kupata bao kutokana na kuokoa michomo mingi iliyoelekezwa langoni mwake.

Yanga: Ally Mustapha ‘Barthez’, Juma Abdul. Oscar Joshua/Athumani Idd ‘Chuji’, Nadir Haroub, Kelvi Yondani, Mbuyu Twite, Nizar Khalfan/ Hamisi Kiiza, Haruna Niyonzima, Said Bahanunzi, Didier Kavumbagu na Stephano Mwasika.

Prisons: David Abdallah, Henry Mwalugala, Laurian Mpalile, Lugano Mwagama, David Mwanyika, Khalid Fupi, Sino Agustino, Fredy Chufu, Elias Maguli, Peter Michael na Ramadhan Kutoka Bukoba Mwandishi Wetu anaripoti kuwa Azam FC jana ilianza vyema ligi hiyo baada ya kuifunga Kagera Sugar bao 1-0 kwenye Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba.

Mpira wa kona uliopigwa na Erasto Nyoni dakika ya 55 ulitua kichwani mwa Abdulhalim Homoud aliyeukwamisha wavuni na kuandika bao hilo pekee katika mchezo huo.

Kwenye Uwanja wa Mkwakwani Tanga, timu ya Coastal Union nayo ilikaribisha Mgambo JKT kwa kuifunga bao 1-0 Uwanja wa Mkwakwani Tanga. Bao la Coastal Union lilifungwa dakika ya 46 na Jerry Santo baada ya kupokea pasi ya Juma Jabu.

Mgambo ni miongoni mwa timu mpya katika msimu wa Ligi Kuu Tanzania Bara, ambapo timu nyingine zilizopanda daraja ni Polisi Morogoro na Prisons.

Mchezo mwingine wa ligi hiyo ulifanyika Uwanja wa Azam Chamazi, ambapo JKT Ruvu iliifunga Ruvu Shooting mabao 2-1. Mabao ya washindi yalifungwa na Said Ortega na Omari Changa wakati lile la Ruvu Shooting lilifungwa na Hassan Dilunga.

Habari zilizopatikana kutoka Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza ni kuwa timu ya Toto Africans na JKT Oljoro zilifungana bao 1-1 jana.

Kutoka Morogoro John Nditi anaripoti kuwa Mtibwa Sugar na Polisi Morogoro jana zilishindwa kufungana katika mfululizo wa ligi hiyo mchezo uliofanyika Uwanja wa Jamhuri.