23Mei2013

 

Coastal wachekelea Prisons kuikomalia Yanga

KOCHA wa Coastal Union ya Tanga, Juma Mgunda amesema kitendo cha Prisons ya hapa kuikomalia Yanga katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara Jumamosi iliyopita kinadhihirisha timu zimejiandaa kwa ushindani.

Yanga licha ya kufanya usajili wa kutisha ulioigharimu fedha nyingi, ilitoka suluhu na Prisons katika moja ya mechi za ufunguzi wa ligi hiyo uliofanyika kwenye Uwanja wa Sokoine jijini hapa.

Akizungumza jijini hapa juzi baada ya mazoezi ya timu yake ambayo leo itakwaana na Prisons katika mchezo wa ligi hiyo, Mgunda alisema Prisons imedhihirisha timu zimejiandaa vizuri kwa ligi hiyo.

“Kwa kweli Prisons pamoja na kupanda daraja na kufanya usajili wa kawaida imedhihirisha kuwa timu zimejiandaa vizuri kwa ligi hiyo na hakuna lelemama, “alisema Mgunda. Katika mchezo huo, wachezaji wa Prisons waliwafunika kwa kiasi kikubwa nyota wa Yanga kiasi cha kutoonekana kabisa licha ya kuingia uwanjani kwa mbwembwe nyingi. Mgunda akizungumzia mchezo wao wa leo dhidi ya Prisons alikiri utakuwa mgumu huku akisisitiza wamejiandaa kufanya vizuri katika mchezo huo. “Mchezo utakuwa mgumu lakini tumejiandaa kufanya vizuri dhidi ya Prisons,“ alisema Mgunda. Akizungumzia hali ya sehemu ya kuchezea ya uwanja huo, Mgunda alipongeza kwa angalau kuwa na nyasi, lakini aliwataka wamiliki wake kushirikiana na wadau wa soka mkoa wa Mbeya kuboresha zaidi sehemu hiyo. “Sehemu ya kuchezea pamoja na kuwa bora kidogo ukilinganisha ilivyokuwa miaka mitatu iliyopita, lakini bado wahusika wanatakiwa kushirikiana na viongozi wa soka Mbeya ili kuzidi kuiboresha sehemu hiyo,“ alisema.