Mambo yaiva usaili video ya Diamond
- Imeandikwa tarehe 19 Septemba 2012
- By Mwandishi Wetu
- Imesomwa mara: 363
USAILI wa wanamitindo na wachezaji watakaonekana kwenye video mpya ya msanii wa Kimataifa wa Tanzania, Naseeb Abdul ‘Diamond Platnumz’ unatarajiwa kufanyika ukumbi wa Nyumbani Lounge, Kinondoni, Dar es Salaam.
Akizungumza mjini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Kampuni ya One Touch Solutions, Petter Mwendapole alisema wamechagua Nyumbani Lounge kwa kuwa ni rahisi kufikika na watu wengi.
“Nyumbani lounge inamilikiwa na msanii mwingine wa kimataifa wa Tanzania, Judith Wambura Mbibo ‘Lady Jaydee’, na huyu ni msanii wa kwanza kuweza kusimama mwenyewe na kujitegemea, mchango wake ni mkubwa katika ulimwengu wa muziki wa kizazi kipya Tanzania, wanaohitajika kuja kwenye usaili pia tunatarajia watakuja kujitegemea kwa kufuata nyayo za JD,” alisema.
Mwendapole alisema, uongozi wa Nyumbani Lounge chini ya Mkurugenzi wake, Gadner G Habash ulipopewa wazo la kufanyika usaili huo hawakusita na walipokea kwa mikono miwili na kuahidi kushirikiana na timu nzima ya Diamond katika kuhakikisha usaili huo unafanikiwa.
Mkurugenzi huyo pia alisema watu wengi wamekuwa wakiuliza maswali kuhusu malipo na vigezo ambavyo vitatumika katika kuwapata watu watakaoshiriki kwenye usaili huo ambapo alieleza kuwa watakaochaguliwa watalipwa na ndio maana kumewekwa usaili.
“Wote watakaochaguliwa kuonekana kwenye video hiyo watalipwa, mpango wa Diamond ni kutengeneza ajira kwa watu wengine si kuuza sura kama watu wengi wanavyowaita wale wanaonekana kwenye video, vigezo pale kutakuwa wabunifu wa mitindo ambao wamesomea kazi zao, kutakuwa na walimu wa muziki, kutakuwa na watu ambao wamesomea mambo ya uongozaji wa picha na kurekodi, hii timu itaangalia vitu vingi kupata washindi,” alisema.


