Kumsamehe mwenza wako ni upendo wa kweli
- Imeandikwa tarehe 02 Septemba 2012
- By Halima Mlacha
- Imesomwa mara: 1214
KUSAMEHE mtu ni moja ya dalili nzuri ya maadili, na kwa kusisitiza kila dini inafundisha juu ya umuhimu wa kusamehe.
Hata hivyo, pamoja na kufundishwa katika dini na hata na wazazi wetu bado watu wengi huwawia vigumu kuwasamehe wale waliowakosea.
Msamaha huhusishwa kwa karibu sana na aina ya kosa lililofanywa na mkosaji lakini kubwa zaidi ni uhusiano wa mkosaji na aliyekosewa.
Ni rahisi sana kutoa msamaha kwa makosa madogomadogo kwa sababu hayana madhara makubwa kutokana na urahisi wake wa kuyasahau.
Lakini pamoja na hayo kuna baadhi ya watu hata makosa madogo kama hayo huwawia vigumu kuyasamehe kutokana na ukaribu, thamani, heshima na imani waliyokuwa nayo juu ya mtu aliyewakosea.
Hali hiyo haina tofauti kabisa katika suala la uhusiano wa kimapenzi, wenza hukoseana sana tena wakati mwingine hufanya makosa mara kwa mara lakini msamaha ndio silaha kubwa ya kuimarisha uhusiano huo.
Katika uhusiano kama mwenza wako amekukosea itakuwa rahisi sana kama utamsamehe na kusahau yote. Na la maana sana ni kusahau na kusamehe kwa dhati, si baadae unaanza manung’uniko.
Hakuna kitu kibaya ambacho kinaweza kuharibu uhusiano kama mtakuwa mmekoseana au umekosewa na mwenza wako akakuomba msamaha, ukajibu umesahau lakini ukawa hujasahau.
Kama unaamua kusamehe ni vyema ukajaribu kufanya vitu ambavyo vitakusaidia kusahau tukio zima la sivyo utajikuta ukirudi kule kule kwenye kosa na kuharibu kila kitu.
Katika uhusiano wowote, suala la msamaha ni muhimu na la lazima ili kuujengea mizizi uhusiano wenu, ni lazima tukubaliane kuwa makosa ni moja ya mambo ambayo yapo na yanayotokea katika maisha yetu na kwamba kila mmoja anaweza kuyafanya.
Ni wazi kuwa mwanzoni utajisikia hasira sana, utazungumza yote na hata kutishia kuondoka nakadhalika, lakini baada ya muda hasira zako zitakapopungua jaribu kujenga mazingitra ya kulisahau tukio zima kama umeamua kumsaheme aliyekukosea.
Hivyo ndivyo inavyotakiwa hata katika uhusiano, pamoja na hasira utakazokuwa nazo au namna utakavyojisikia kuwa umesalitiwa kadri muda unavyokwenda na hasa mkosaji anapojitolea kuomba msamaha ndivyo hasira zinapopungua na kulisahau tukio zima.
Sisemi kuwa ni rahisi kusahau kwani hapa pia inabidi aina ya kosa lenyewe liangaliwe, kinachosisitizwa ni kwamba pamoja na ukubwa wa kosa, bila kujali muda utakaochukua ni lazima tujifunze kusamehe.
Ugumu wa kusamehe huja pale inapotokea kuwa mwenza wako ambaye ulikuwa karibu naye sana anafanya jambo ambalo litakustua na kukuumiza vibaya moyo wako.
Hali hiyo mara nyingi huwa si rahisi kusamehe, matokeo yake huwa kwanza ni kutokuamini kama ni kweli imetokea, mkosewaji hujikuta akijiuliza maswali mengi na hatma ya uhusiano huwa mashakani.
Mara nyingi katika uhusiano inapotokea tatizo kama hilo, huchukua muda mrefu sana kwa mkosewaji kufiria suala la msamaha licha tu ya kusahau.
Baadhi ya watu wanaweza wasiwasamehe wenza wao kabisa kwa makosa makubwa kama vile kutokuwa waaminifu kwenye uhusiano, huwa si rahisi kwa kosa kama hilo kusamehe.
Lakini tunapaswa tutambue kuwa hata kama kosa ni kubwa vipi, hatuwezi kuendelea na maisha yetu kama hatutajifunza kusamehe.
Maisha ni mzunguko, ni lazima tukubali kuwa ni lazima tusahau hata kama tukishindwa kusamehe ili tuweze kupata amani ya moyo.
Kwa ushauri zaidi au mapendekezo wasiliana nasi kupitia tovuti ya This email address is being protected from spambots. You need JavaScript enabled to view it. au This email address is being protected from spambots. You need JavaScript enabled to view it.


