19Mei2013

 

POROJO ZA ANKO SAGATI: Utamu wa sigara, pombe na kitimoto!

HEBU fikiria una mpenzi anayenuka mdomo, hivi utamwambia ukweli kuwa unanuka mdomo?

Au utakaa kimya ila utakuwa unakwepa busu lake la mdomo? Sasa hapo raha ya mapenzi iko wapi? Raha ya mapenzi ni kila mtu awe huru na mwenzake.

Juzi Daktari mkongwe Ali Mzige alitoa mhadhara katika chumba chetu cha habari na kusema Watanzania wengi wananuka vinywa vyao.

Nimemwita mkongwe kwa maana amekuwa Mkurugenzi wa Kinga na Tiba katika Wizara ya Afya kwa miaka mingi hadi kustaafu kwake miaka ya hivi karibuni.

Akasema tunanuka vinywa vyetu kwa sababu hatuzingatii kanuni za usafi wa kinywa. Tumekariri kupiga mswaki asubuhi lakini tunapojiandaa kwenda kitandani jioni hatuna mpango na vinywa vyetu.

Kwa hali hiyo yale mabaki ya chakula yanafanya mdomo kunuka hata kama ukipiga mswaki asubuhi hakuna kitakachosaidia kuepukana na harufu mbaya yam domo.

Hebu jiulize mara ngapi unapotaka kwenda kulala unapiga mswaki au ukishaoga unawaza kitanda. Yaani tumekuwa mabingwa wa kuoga hata kama kuna baridi kiasi gani, lakini tunasahau kuosha sehemu ya mwili wetu ambayo ni mdomo wako, kiungo muhimu sana kwa kupokea chakula na kufanya shughuli zingine nyingi tu ikiwa ni pamoja na kuonja mapishi.

Matokeo ya dharau hizo ndio hayo tuliyoambiwa na daktari huyu, mdomo kunuka na wakati mwingine unaona aibu hata kuzungumza mbele za watu kutokana na harufu mbaya inayotema kutoka mdomoni.

Kazi kwenu ndugu zangu, kama unataka kuendelea kunuka mdomo dharau ushauri wa bingwa huyu ila kama unahitaji kufurahi mbele ya kadamnasi ya watu ni vyema tuanze kutunza vinywa vyetu.

Daktari huyu hakuishia hapa, akaendelea kutoboa kuwa kwa wale wanaopenda kilevi cha pombe, akasema wana uwezekano wa kupata magonjwa 60 ikiwa ni pamoja na kupunguza kinga za mwili maarufu kama CD4. Nikafikiria namna ambavyo wabongo baada ya kazi wanavyopenda kujimwaga kwenye vilinge kwa ajili ya kupata moja baridi na moja moto wakati tunasubiri kupungua kwa foleni za jiji letu na kwenye miji mingine. Haishii hapo, wavuta sigara sasa hawa nao magonjwa 40 yanawanyemelea ambayo ni hatari kwa afya zao na mojawapo ni kupata magonjwa ya jamii ya saratani na upungufu wa nguvu za kiume. Ohoo kumbe kama unataka kuwa mgumba, weye endekeza sigara. Kwa wale walevi wa ngono, hawa nao hawako salama sio kupata Ukimwi tu na kaswende, wao wako katika hatari ya kupata magonjwa 23 ambayo pia ni hatari kwa afya zao. Maana hata vitabu vya biblia vimesema adhabu ya zinaa iko juu ya mwili wako mwenyewe. Na nyama ya kitimoto je? Hapa ndo usiseme. Nasikia mbuzi katoliki huyu ni hatari zaidi kwa afya yako. Yeye anaweza kuambukiza magonjwa zaidi ya 17. Sasa fikiria mtu anakunywa pombe ana magonjwa 60, kama unavuta sigara magonjwa 40, zinaa magonjwa 23 na kama unatumia kiti moto una magonjwa 17 hivi mwili wako kweli ni salama? Utakuwaje salama wakati una jumla ya magonjwa 140! Kazi kwako wewe mnywa pombe, mvuta sigara, mwendekeza ngono na mtumiaji wa kitimoto. Acha mara moja utaishi salama.