KAMA MZAZI:Mchelea mwana kulia hulia yeye
- Imeandikwa tarehe 08 Machi 2013
- By Nicodemus Ikonko
- Imesomwa mara: 397
AMA kweli msemo wa wahenga usemao ‘Mchelea mwana kulia hulia yeye’ ndiyo unaolikumba taifa la Tanzania hivi sasa baada ya Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa, kutangaza hivi karibuni matokeo ya kidato cha nne ya mwaka 2012.
Sina haja ya kurudia takwimu zote za matokeo hayo bali itoshe tu kusema kwamba zaidi ya wanafunzi 240,000, sawa na asilimia zaidi ya 60 ya waliofanya mtihani huo wamepata alama sifuri. Hakuna kitu. Hawatapata hata cheti. Makubwa haya. Kila mmoja analia. Tangu wazazi, wanafunzi, ndugu, jamaa na marafiki. Tumeguswa kila mmoja kwa nafasi yake.
Tayari imeripotiwa katika vyombo vya habari kuwa wanafunzi wapatao watatu ni miongoni mwa wahitimu waliochukua hatua isiyotarajiwa ya kumaliza maisha yao kwa kujiua.
Kweli sasa tunalia! Sababu lukuki za wanafunzi kufeli zimetolewa na wanajamii mbalimbali, ikiwa ni pamoja na ubora hafifu wa baadhi ya walimu, ukosefu wa maabara kwa masomo ya sayansi, wanafunzi hao kutofanya mtihani wa kidato cha pili ili kuchujwa kabla ya kuingia kidato cha tatu na maslahi duni kwa walimu.
Tunazo sababu nyingi kwelikweli. Lakini mimi Kama Mzazi licha ya kuzikubali sababu hizo nalia na wazazi wenzangu! Tumechelea mno kulia kwa watoto wetu kwa maana kwamba tumewaachia waendeshe ratiba zao za maisha kama wanavyotaka wao na siyo sisi wazazi kuwawekea ratiba elekezi.
Mwanafunzi akisharudi nyumbani tu na kupata chakula au chochote kile akala, wazo linalomjia kichwani ni kwenda sebuleni kujikita kwenye vipindi vyao mbalimbali vya televisheni ikiwemo michezo ya kuigiza, mpira, sinema mbalimbali za Kiafrika, Kihindi, Kichina na nyingine lukuki za Ulaya.
Watoto hawa wa shule, na hapa nitaongelea zaidi wa mijini, hawana habari na kazi walizopewa na mwalimu wala kujiandaa kwa vipindi vya kesho yake.
Ukifika wakati wa kujiandaa kwa majaribio ya mwezi au mitihani ya kumaliza mihula, huwezi kuona tofauti kati ya alipoanza muhula na wakati wa maandalizi hayo kwani ratiba yake ni ileile.
Hakuna dalili za kufanya marejeo ya masomo yake ili kuwa tayari kwa mitihani hiyo wala kuona anavyohangaika kutafuta kujua yale ambayo hayajui ama kasahau.
Usiku nako usiseme hizo simu za viganjani nazo zina nafasi yake. Kutumiana ujumbe, kulonga usiku kucha na marafiki zao. Wakiamka asubuhi huelemewa na usingizi, kisa alikuwa anakesha kwa kulonga na rafiki zake.
Hivi wazazi tujiulize, gharama za kuwasomesha tunatoa sisi, televisheni za kwetu, simu tumewanunulia sisi, fedha za kuweka vocha huwapatia sisi lakini hatuwapatii ratiba elekezi kuwaongoza katika kufuatilia maisha yao ya shule.
Sisemi kwamba wazazi wote hukaa kimya na kuwaachia watoto wafanye wanavyotaka, lakini hali halisi ni kwamba tunasema huku tukiwa hatufuatilii utekelezaji wa maelekezo yetu.
Ni kweli, tupo katika kizazi cha utandawazi ambacho wengine wanakiita cha dot com, lakini uwepo wa wingi wa vyombo vya habari na teknolojia ya mawasiliano haiwezi kuwa sababu ya kuwaacha watoto wetu waogelee katika bahari hii ya maisha kama wapendavyo kwa kujiongoza na ratiba zao.
Mimi nadhani huu ndio wakati ambao tulitakiwa kuwa makini zaidi. Kukamilika kwa mwanafunzi ni pamoja na kufuata ratiba ya masomo yake darasani, kucheza michezo mbalimbali ikiwa ni pamoja na mpira, riadha, michezo ya kuigiza, utamaduni, stadi za kazi pamoja na kazi ndogo ndogo kama za kufanya usafi, kumwagilia bustani na nyinginezo, ndipo mtoto atakuwa anakamilika katika masomo yake.
Kwa bahati mbaya hali ilivyo sasa wazazi na walezi tumewapatia wototo wetu taswira kwamba maisha ni ‘burudani tu’ tangu asubuhi hadi jioni. Ikifika siku za mwisho wa wiki, yaani Jumamosi na Jumapili, basi ni burudani kwa kwenda mbele kama vile hakuna lingine la kuweza kufanya. Hebu fikiria hili.
Kwamba sisi wazazi na walezi tulioko katika ajira, tumewekewa wasimamizi wa kazi ama mabosi kama ambavyo wengi wangeita. Kila mwajiriwa anasimamiwa na mkurugenzi, mhariri, mwalimu mkuu, ofisa utawala, mkuu wa wilaya, mkuu wa mkoa, waziri, bodi ya wakurugenzi na kadhalika.
Kama tunasimamiwa ndivyo, na nafasi nyingine ili kutusimamia na kutuongoza katika utekelezaji wa kazi zetu, iwaje tuamini kwamba watoto wetu chini ya miaka 18 waweze kujiongoza wenyewe? Huku ni kujidanganya.
Tuchukue nafasi zetu kwa kuwapatia watoto wetu ratiba elekezi na kuiisimamia ipasavyo. Mchelea mwana kulia hulia yeye! Alamsiki. Nicodemus Ikonko This email address is being protected from spambots. You need JavaScript enabled to view it. 0766 843382


