18Mei2013

 

Siasa isitupotezee muda wa maendeleo

KAUL I ya Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo kwa Watanzania kushindwa kuendelea kiuchumi kutokana na muda wao wa kazi ili kuinua kipato kuupotezea kwenye siasa za kuzungumzia watu, inapaswa kuungwa mkono na kufanyiwa kazi.

Profesa Muhongo amehadharisha kuwa kama hali hii itaachwa iendelee kama ilivyo sasa, Watanzania kamwe hawataweza kukimbizana na nchi nyingine, kwani hawatumii muda wao inavyopasa katika kukabiliana na umasikini.

Waziri Muhongo ametoa kauli hiyo kwa wakati mwafaka, ambao viongozi wa siasa wako barabarani wakieneza na kuelimisha wananchi kuhusu sera za vyama vyao huku wengine wakitumia fursa hiyo kuhamasisha wananchi kupinga shughuli za maendeleo.

Wananchi wenye vichwa vyepesi wasiotaka kutafakari na kujiuliza, nao wamekuwa wakiyumbishwa na kufuata upepo kama bendera na kususia shughuli za kiuchumi bila kujali kuwa ndizo zinazoweza kuwakomboa na kuondokana na umasikini walionao.

Viongozi wa kisiasa nchi hii wana bahati ya kusikilizwa na wananchi ambao kwa miaka nenda rudi hawana hulka ya ukaidi, na hivyo wameweka imani kwa wanasiasa kwa kila wanachokisema na matokeo yake ni kutopea katika umasikini kama ilivyo sasa.

Mathalani Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari (Chadema), alikaririwa hivi karibuni na vyombo vya habari, akishawishi wananchi kususa mbio za Mwenge wa Uhuru, kwa madai kuwa zimekuwa hazina tija na badala yake zinatumia fedha nyingi bila faida kwa wananchi.

Nassari, ambaye ni mbunge mpya, akasema hataki kuona Mwenge ukiingia jimboni mwake, kwa sababu hizo alizozitoa bila kuzingatia kuwa mbio hizo zimekuwa na tija kwa kuzindua miradi mbalimbali ya maendeleo kwa wananchi.

Hata kama Nassari haupendi Mwenge kwa sababu tu unasimamiwa na Serikali iliyoko madarakani, lakini akumbuke, kuwa ‘Baniani mbaya kiatu chake dawa’; mbio za Mwenge zinatumika kama njia ya kuhamasisha wananchi kushirikiana na Serikali yao kujiletea maendeleo na si vinginevyo.

Huo ni mfano mojawapo unaoonesha jinsi wanasiasa wasivyozingatia maendeleo ya wananchi wao na badala yake wanatanguliza chuki na kuzipandikiza kwa wananchi, ili waone na kuamini, kwamba Serikali yao hakuna inachokifanya zaidi ya ubadhirifu kupitia Mwenge.

Kiongozi kama huyu anapoona jambo dogo kama matendo ya ngono katika mbio hizo na kudhani ndicho kikwazo cha maendeleo badala ya kulinganisha vitendo vya kimaendeleo vinavyofanyika sambamba na shughuli za Mwenge, bila shaka anakuwa amepungukiwa busara fulani katika kuchambua mambo.

Vitendo vya ngono katika mikusanyiko ya mikesha ya Mwenge hata kama vipo, havina itikadi bali hulka ya binadamu na haviwezi kufanyika kwa kiwango kikubwa mpaka cha kufunika hata shughuli za uzinduaji miradi ya wananchi ambalo ndilo lengo hasa la mbio hizo.

Ikumbukwe, kwamba mikesha ya Mwenge haina tofauti na shughuli zingine za kibinadamu zinazofanywa kwa staili hiyo, zikiwamo za harusi na sherehe zingine zinazofanyika usiku ambazo huendana na shamrashamra kadhaa na matukio kama hayo kujitokeza kutegemea na tabia za watu.

Hadhari ya Profesa Muhongo inapaswa kuchukuliwa kwa uzito wake na kufanyiwa kazi, ili viongozi wa kisiasa waone aibu ya kupotosha wananchi na badala yake waungane na Serikali katika kuimba wimbo mmoja wa maendeleo.

Na kama alivyosisitiza, Serikali imedhamiria kumaliza umasikini wa wananchi wake kwa kutoa huduma ya umeme wa uhakika, hali itakayosaidia kuinua uchumi wa Taifa na kuwa katika ushindani mzuri wa kibiashara kati ya nchi zinazoendelea. Hiyo ndiyo inapaswa kuwa kaulimbiu ya wanasiasa wote.