25Mei2013

 

Hongera Mukangara, TFF mtumie busara sasa

MWANZONI wa wiki hii, Serikali kupitia kwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo, Dk Fenella Mukangara, ilitangaza kuagiza kufutwa kwa matumizi ya Katiba ya Shirikisho la Soka la Tanzania (TFF) ya mwaka 2012, kwa kuwa imekiuka Kanuni na Sheria ya Baraza la Michezo la Taifa (BMT).

Kwa mujibu wa Mukangara, Uchaguzi Mkuu wa TFF unatakiwa kufanyika chini ya Katiba ya zamani ya mwaka 2006, na siyo ya mwaka 2012, iliyopitishwa kwa njia ya waraka na kulalamikiwa na wadau.

Amesema kuwa shirikisho hilo la soka Tanzania limekiuka Sheria Namba 12 ya BMT na marekebisho yake Namba 6 ya mwaka 1971 pamoja na Kanuni za Usajili Namba 442 za mwaka 1999.

“Kanuni ya BMT Namba 11(1) inaeleza wazi utaratibu wa marekebisho ya Katiba ambapo walitakiwa wajaze Fomu Namba 6, 7, 8 na 9 kisha baada ya siku 14, Msajili wa Vyama vya Michezo anatakiwa kuwajibu, kama anakubali anatumia Fomu Namba 11 na kama anakataa anatumia Fomu Namba 10, lakini TFF walikiuka yote haya,” alifafanua Dk Mukangara, Jumatatu wiki hii alipozungumza na wanahabari.

Mbali ya kuiagiza TFF kufanya uchaguzi wa viongozi kwa mujibu wa Katiba ya mwaka 2006, alisema kama kuna umuhimu wa kurekebisha Katiba, waitishe Mkutano Mkuu kwa kufuata misingi ya Katiba yao ya mwaka 2006 na Kanuni za BMT kwa ajili ya kufanya maboresho hayo.

Awali ya yote, tunampongeza Dk Mukangara kwa kuona umuhimu wa Wizara yake kwa kutumia taasisi zilizo chini yake na zilizopewa mamlaka kisheria, kuingilia kati na kuweka sawa masuala ya Katiba ya TFF ambayo ni moja ya eneo lililolalamikiwa na wadau wakati wa mchakato wa uchaguzi wa TFF ambao sasa umesimamishwa baada ya kugubikwa na mizengwe na malalamiko kadhaa.

Ni uamuzi wa busara unaopaswa kupongezwa kwa sababu Serikali kama msimamizi wa michezo nchini imeona udhaifu wa Katiba ya TFF kwa kukiuka kanuni na sheria za nchi zinazoongoza michezo, hivyo bila kusita, akaingilia kati ili kunusuru ukiukwaji huo wa sheria usiendelee.

Tunampongeza Waziri kwa hili. Lakini wakati tukimpongeza, tunawaomba wadau wa michezo hasa soka nchini, kuelewa kuwa uamuzi wa Waziri haujakiuka kanuni wala sheria yoyote kiasi cha kuwapo hisia za tishio la Tanzania kufungiwa na FIFA kwa kile kilichozoeleka kuwa ni Serikali kuingilia masuala ya michezo.

Alichofanya Waziri ni kusimamia sheria za nchi zinavyoeleza katika kuendesha michezo nchini, kama ambavyo FIFA inafanya kuheshimu sheria za Uswisi ambako ndiko yaliko makao makuu yake.

TFF kwa mujibu wa sheria za nchi, inao wajibu wa kuutekeleza kwa BMT na Msajili wa Vyama vya Michezo nchini hasa linapokuja suala la Katiba. Kwa hiyo, hakuna kilichokwenda kinyume.

Lingine la muhimu ni kwa wakuu wa TFF wanaokutana leo chini ya uenyekiti wa Rais wao, Leodegar Tenga kuona busara ya kuhakikisha suala hili la Katiba linamalizika kwa haraka kama Serikali ilivyoagiza na kupisha mchakato wa Uchaguzi Mkuu uweze kuendelea.