23Mei2013

 

Tume ya Kidato cha Nne ipewe ushirikiano

TUME ya Taifa ya Kuchunguza Matokeo ya Kidato cha Nne, imeshatangazwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda na ameipa muda wa wiki sita kuanzia wiki hii, kumaliza kazi iliyo mbele yao.

Pinda wakati akitangaza Tume hiyo inayoongozwa na Katibu Mtendaji wa Tume ya Vyuo Vikuu (TCU), Profesa Sifuni Mchome, aliagiza pamoja na mambo mengine, sababu za matokeo mabaya ya kidato cha nne yaliyotangazwa mwaka huu, zibainishwe.

Pia aliagiza Tume hiyo itoe mapendekezo ya hatua za kuchukua mara moja kwa wanafunzi 240,903, waliopata daraja sifuri katika mtihani huo uliofanyika mwaka jana na hatua za kukabiliana na tatizo la kushuka kwa kiwango cha elimu nchini.

Tayari Rais Jakaya Kikwete katika hotuba yake ya mwisho wa mwezi uliopita, alisema lazima ukweli kuhusu matokeo hayo ujulikane kwa uhakika.

Katika hotuba hiyo, Rais Kikwete aliomba kila mtu mwenye mawazo yake, ayafikishe kwenye Tume hiyo ili jawabu muafaka la tatizo hili lipatikane.

Tunaipongeza Serikali kwa kuendelea kuwa sikivu na kuwa sehemu ya wananchi, kwa kushirikiana nao katika kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazojitokeza na kutoa uzito unaostahili katika suala hili.

Tunafahamu suala la elimu ni muhimu katika jamii yoyote na ni ukweli usiopingika kuwa Serikali imekuwa ikizingatia umuhimu huo kwa Watanzania.

Tunasema hivyo kwa kuwa ushahidi uko wazi katika ongezeko la shule za sekondari na udahili wa wanafunzi, ongezeko la vyuo vya elimu ya juu na ongezeko la udahili wa walimu katika vyuo hivyo.

Hatuwezi kubeza jitihada za Serikali katika kuboresha elimu ya Tanzania mpaka tumefikia hatua tunatarajia katika miaka si mingi, shule za msingi zifundishwe na walimu wenye shahada.

Tunajua ipo changamoto ya walimu wa sayansi inayotokana pia na mwamko mdogo wa jamii yetu katika kupenda masomo hayo, unaochangiwa pia na dhana potofu kwamba masomo hayo ni magumu.

Hata hivyo pamoja na changamoto hizo, Serikali imeendelea kukabiliana nazo na mfano mzuri ni uamuzi wa kutenga bajeti ya elimu ya Sh trilioni 3.6, ambayo ni sawa na asilimia 24 ya bajeti yote ya Serikali na ndiyo kubwa kuliko zote.

Rais Kikwete katika hotuba yake ya mwisho wa mwezi, alisema wametenga bajeti hiyo kubwa katika elimu, ili iwezeshe kuendelea kukabiliana na mahitaji na changamoto za upanuzi mkubwa wa elimu ya sekondari na elimu ya juu.

Tunashauri Watanzania kutoingiza siasa za kujitafutia umaarufu katika hili na wote wenye maoni, kama Rais Kikwete alivyowaomba, watoe ushirikiano wa kutosha kwa Tume.

Haitakuwa na maana kuendeleza siasa za kusubiri hitilafu itokee, ndiyo tutoe maoni yenye asili ya malalamiko, kwa malengo yasiyo ya kizalendo ya kutaka Serikali ionekane imeshindwa kazi au chama fulani, au mwanasiasa fulani apoteze mvuto na kingine au mwanasiasa mwingine ajiongezee mvuto.

Elimu hii ni kwa ajili yetu sote bila kujali itikadi ya vyama vya siasa wala dini na ni kwa ajili ya msingi wa kizazi kijacho. Ndio maana tunasisitiza mwenye maoni atoe ushirikiano wa kutosha kwa Tume.