WANACHUO 500 wahitimu mwaka huu wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (Saut) cha jijini hapa wamefeli mitihani yao ya mwisho kwenye kozi mbalimbali.
Hayo yalisemwa jana jijini hapa na Makamu Mkuu wa Saut, Dk Charles Kitima kwenye hotuba yake ya ufunguzi wa mahafali ya 14 ya chuo hicho.
Dk Kitima alisema wanafunzi hao ni kati ya wahitimu 3,044 waliotunukiwa vyeti vyao jana na walishindwa kwenye mitihani kutokana na kukosa kukidhi mahitaji ya kitaaluma kwa mujibu wa sheria ya mitihani ya vyuo vikuu nchini.
“Zaidi ya wanafunzi 500 hawatatunukiwa vyeti vyao leo kutokana na kutokidhi vigezo vya mahitaji ya kitaaluma, hawa watarudia,” alisema.
Dk Kitima alisema kati ya wahitimu waliotunukiwa vyeti jana, ni mmoja tu aliyepata daraja la kwanza kutoka Idara ya Uchumi, huku wengi wakipata daraja la pili na wachache la tatu.
Hata hivyo, alisema huenda kushindwa kwa wanafunzi hao kunatokana na Serikali kutowekeza katika sekta ya elimu ya juu, hali ambayo inafanya kiwango cha elimu hiyo kushuka.
“Elimu ya juu nchini bado iko chini, hii inatokana na serikali kuwa na uwekezaji mdogo katika elimu ya juu hali hii haitoi fursa kwa watoto wa wanyonge hasa wakulima kupata fursa ya kusoma,” alifafanua.
Alisema Saut kwa kuthamini umuhimu wa elimu ya juu kwa watoto wa wakulima na wasiokuwa na uwezo, inasomesha watoto 80 kwa ruzuku yake.
“Sisi kwa kutumia fedha za Chuo tunasomesha vijana 80 hapa, leo hii nendeni Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kama mtakuta vijana wa masikini wanasomeshwa na fedha za chuo, sisi tumedhamiria kutumikia Watanzania kuwapa elimu bora hasa waishio vijijini,” alifafanua.
Aliitaka Serikali kutoa ajira kwa wanafunzi wa vyuo vikuu wanaohitimu kozi zao ili wasiendelee kukaa mitaani. Akitoa mfano, alisema mwaka jana jumla ya wahitimu 1,000 wa Shahada ya Elimu wako mitaani bila ajira.
“Vijana hawa walipokwenda kuomba ajira wakaambiwa wasubiri mwezi wa kwanza, ni nchi gani makini ya kufanya uzembe huu wa kutoajiri vijana hawa kama si Tanzania?” Alihoji na kuitaka serikali kuona uwezekano wa kuajiri wahitimu hao.
Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli ambaye alikuwa mgeni rasmi, aliutaka uongozi wa chuo hicho, kufanya kila linalowezekana kuhakikisha kuwa wanafunzi hao walioshindwa mitihani wanafaulu vema kwa mitihani ya marudio.
“Tunaamini Saut mtafanya kila linalowezekana, maana chuo hiki ni cha kiroho, kina viongozi wa kiroho, mtaweka bidii zaidi ili vijana hawa waliofeli ili wanafaulu mitihani yao,” alisema.