20Mei2013

 

Juhudi za DC Handeni ziungwe mkono

JANA kulikuwa na taarifa katika vyombo vya habari zikimhusu Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Muhingo Rweyemamu, akielezewa kusambaratisha ndoa ya mwanafunzi wa kidato cha kwanza iliyodumu kwa siku tatu.

Tukio hili si la kwanza tangu kuchaguliwa kuongoza wilaya hiyo, Rweyemamu amenusuru wanafunzi kadhaa walioachishwa shule kwa lengo la kwenda kuozeshwa na kuvuruga mipango mingi ya ndoa kama hizo, ambazo waathirika wakubwa ni wanafunzi wa kike.

Ukiangalia kwa mapana yake, tatizo la wanafunzi wa kike walio na umri wa kati ya miaka 12 na 16 kulazimishwa kuolewa, si tatizo la Handeni pekee bali ni la kitaifa ambalo linajitokeza katika mikoa mingi nchini na kuathiri zaidi watoto wa kike.

Pia kuna sababu nyingine ambazo zinafanya wanafunzi hususan wa kike kukatishwa masomo licha ya juhudi za Serikali kutaka kila mtoto mwenye umri wa kwenda shule apate elimu ya msingi hadi sekondari kwa usawa bila kujali kipato cha familia husika.

Baadhi ya sababu zinazochangia tatizo la wanafunzi kuacha shule nchini, ni pamoja na umasikini wa wazazi, kupata ujauzito, mila na desturi za baadhi ya makabila, mazingira magumu ya shule ukiwamo umbali kutoka nyumbani hadi shuleni, migogoro ya kifamilia, vishawishi na tamaa za wanafunzi wenyewe.

Lakini tatizo la ndoa za lazima kwa watoto au wanafunzi kutoroshwa na wanaume, ni tatizo sugu ambalo jamii inatakiwa kubadilika ili kupambana nalo na kuhakikisha watoto wa kike hawakosi haki yao ya msingi ya kupata elimu ambayo itamsaidia kutoa ujinga na kuendesha familia yake ya baadaye.

Kutokana na tatizo hili, wazazi wengi wamekuwa chanzo cha uharibifu huo, huku wengine hawako tayari kufikisha masuala haya Polisi na hata wanaposaidiwa kufanya hivyo, wasichana na wazazi hawawapi polisi ushirikiano na pia kufanya kuibuka kwa migongano kati ya wazazi na walimu wa wanafunzi hao.

Hivyo kuna haja kwa jamii kuunga mkono juhudi za Mkuu wa Wilaya ya Handeni na Watanzania wengine ambao wako mstari wa mbele kuhakikisha tatizo la wanafunzi kuozeshwa wakiwa na umri mdogo, kuachishwa shule linakoma na watoto wanapata haki zao za msingi za kupata elimu.

Ikumbukwe, kuwa elimu ndicho kitu pekee ambacho mtoto anaweza kurithishwa na wazazi, maana elimu ndiyo itakayofanya tuwe na jamii nzuri ambayo inaweza kuendesha maisha yake bila kuwa na matatizo wanapokuwa wakubwa.

Familia ambazo bado zinaendeleza tabia ya kuwaozesha watoto wao, wajue kwa kufanya hivyo kunachangia kuifanya familia hiyo kuendelea kuwa masikini pamoja na kuwa wanaweza kupewa mahari ambazo kwa wakati huo wanaona ni nyingi, kwani kwa kusomesha mwanamke ni kama umesomesha jamii yote.

Katika kuthibitisha hili ndiyo maana hata vitabu vya dini vimezungumzia suala la watoto kupewa elimu na kutaka watoto hao kushika elimu hiyo kwa manufaa ya vizazi vijavyo. Bila kufanya hivyo kuna hatari ya kuzalisha Taifa lisilofaa, na pia kuna hatari kubwa watoto hao kuanza kuendesha na kujenga familia wakiwa na umri ndogo.

Hivyo juhudi za DC wa Handeni zinatakiwa kuungwa mkono katika kukomesha tatizo hili katika maeneo mengine ili kusaidia Serikali kuhakikisha watoto wote bila kujali jinsia wanapata haki ya msingi ya kupata elimu.