21Mei2013

 

Kwa hili Wizara ya Ujenzi mnastahili pongezi

JUZI Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli alicharuka na kuwataka makandarasi nchini kuhakikisha miradi yao ya ujenzi inafanyika kwa kuzingatia ubora na viwango vya kimataifa, vinginevyo wakiboronga watalazimika kuirudia upya kwa gharama zao.

Na kwa kuonesha kuwa hatanii, alibainisha wazi kuwa tayari makandarasi wawili wa miradi ya ujenzi wa barabara wamerejeshewa barabara walizojenga chini ya kiwango na kutakiwa kuzirudia upya kwa gharama zao.

Barabara hizo ni Sekenke-Shelui yenye urefu wa kilometa 33 iliyoanza kujengwa Februari 11, 2005 na kukabidhiwa kwa Serikali Februari 10, 2007 na barabara ya Nangurukuru-Mbwemkuru yenye urefu wa kilometa 190 ambayo mkataba wake ulisainiwa Februari 2003 na ikakamilika mwishoni mwa mwaka jana, kwa gharama ya Sh bilioni 113.7.

Aidha, wakati akitoa agizo hilo tayari barabara ya Kilwa yenye urefu wa kilometa 5.1 ilijengwa kwa ufadhili wa Serikali ya Japan chini ya mkandarasi aliyeijenga, Kajima inarudiwa upya kujengwa baada ya kuthibitika kuwa imejengwa chini ya kiwango.

Barabara hizo ambazo zilishakabidhiwa kwa Serikali na kuanza kutumika, zimeonekana kuwa chini ya kiwango kutokana na ukweli kuwa hazikuchukua muda mrefu tangu kujengwa na tayari zimeanza kuharibika na kuwa na mashimo.

Ukweli ni kwamba katika nchi yoyote hakuna jambo muhimu kama miundombinu bora ikiwamo barabara ambazo hurahisisha shughuli za kijamii na kiuchumi lakini pia kuunganisha nchi husika na nchi jirani.

Na ndiyo maana Tanzania kama zilivyo nchi nyingine zinazoendelea, iko katika jitihada za kuhakikisha inapata miundombinu bora kwa ajili ya maendeleo ya wananchi na uchumi wake lakini pia kuvutia wawekezaji.

Lakini pamoja na jitihada hizo ambazo zimefanikisha kuwapo kwa miradi ya ujenzi wa barabara katika maeneo tofauti nchini, kumekuwa na makandarasi wanaolipua ujenzi wa barabara na kukwamisha juhudi hizo.

Tumeshuhudia barabara ambazo zinajengwa kwa gharama kubwa zinazotokana na kodi za Watanzania na ufadhili kutoka nje zikijengwa kwa kulipuliwa na matokeo yake baada ya miezi kadhaa huanza kubanduka lami, kujenga mashimo na kupoteza ubora wake.

Hivyo, hatua aliyoamua kuichukua Dk Magufuli na timu yake ya kuwarejeshea miradi makandarasi wanaolipua kazi zao na kujenga upya kwa gharama zao, ni wazi kuwa itakuwa mkwamuzi na mwokozi kwa Watanzania ambao sasa watanufaika vema na barabara za viwango.

Lakini pia suala la kupongezwa zaidi ni hatua za ziada ambazo Waziri huyo amezibainisha juzi kuhusu kusimamisha kazi wahandisi na mameneja wote wanaosimamia miradi itakayothibitika kuborongwa ikiwa ni pamoja na mkandarasi husika kurudia upya ujenzi kwa gharama zake.

Ni wazi kuwa hatua hiyo, itajenga fundisho kwa wote wakiwamo watumishi wasio waaminifu ambao husubiri fedha za miradi mikubwa ya ujenzi kwa ajili ya kujinufaisha na kusababisha miradi hiyo kulipuliwa ni kulisababishia hasara na kadhia Taifa zima la Tanzania.

Ni matarajio yangu kuwa hatua hizo zitachukuliwa kwa uwazi na kuanikwa hadharani kwa makandarasi, wahandisi na mameneja wote watakaobainika kusimamia miradi inayojengwa chini ya kiwango ili iwe fundisho kwao na wengine wenye nia chafu kama hizo.