Wasanii itumieni vyema fursa ya digitali
- Imeandikwa tarehe 02 Machi 2013
- By Evance Ng’ingo
- Imesomwa mara: 262
HIVI karibuni mikoa mbalimbali nchini iliingia katika matumizi ya upatikanaji wa habari kwa njia za kidigitali ambapo wananchi walijikuta wakilazimika kutumia zaidi ving’amuzi ikiwa ndio njia ya kujipatia habari mbalimbali.
Hatua hiyo mbali na kuwa ni muhimu na ya lazima, lakini pia kwa namna moja au nyingine wasanii wa nchini nao wanatakiwa kulitazama suala hilo kwa mtazamo mwingine pia.
Mbali na kuwa kama Watanzania wengine kufurahia, lakini ni watambue kuwa kwa sasa wanakabiliwa na changamoto ya kuboresha kazi zao.
Nasema hivyo kwa kuwa katika ulimwengu huu wa kidigitali, changamoto ni nyingi kwa wasanii kwa kuwa watazamaji wengi ambao ndio mashabiki wao wanapata fursa ya kuziona kazi nyingine nyingi zaidi za wasanii wa nje ya nchi.
Kwa kuwa wasanii wa nchini wakiwa katika analojia walikuwa na uhakika wa kazi zao kuonekana na mashabiki wao wengi na hususan nchini, ila kwa sasa hao watazamaji wanapata fursa ya kuona hata kazi za wasanii wa nje zaidi.
Hata kama pia wakati wa analojia walikuwa wakiziona kazi za wasanii hao wa nje, lakini sasa wanakuwa na fursa zaidi ya kulinganisha kazi za wasanii hao wale wa nje hususan katika ubora wa utengenezaji wa video zao.
Kuna baadhi ya wasanii ambao kwa sasa wanasema kuwa hawawezi kutengeneza video kutokana na kuwa na wasiwasi wa kuhofia kuwa kuwa watazamaji wao wengi hawawaoni kwa sababu hawana ving’amuzi.
Ni vema wasanii hao wakaondokana na mtazamo na kuamua kuwa katika changamoto kama hizo ya kutoonekana na watazamaji wao wasiokuwa na ving’amuzi, ila bado wanatakiwa kutengeneza video zao kwa kiwango cha ubora zaidi.
Nikizungumzia ubora ninamaanisha kuwa umakini wa kazi kuanzia kamera, mavazi, mazingira, wachezaji wazuri pamoja na mengineo muhimu.
Iwapo wakiwa wanatengeneza kazi zao vema na zenye ubora, basi wanakuwa na uhakika kuwa hata wapenzi wa muziki wao waliopo nje ya nchi pia wanaweza kuwaona.
Pia watambue kuwa kwa kujitangaza huko wanaweza kuwa katika mazingira ya kualikwa kufanya maonesho sehemu mbalimbali za nje ya nchi.
Ving’amuzi hivi kwa kuwa vinakuwa vinaangaliwa katika nchi nyingine mbalimbali sasa ndio muda wao katika kuhakikisha kuwa wanawakilisha vema hata huko nje.
Na hili sio kwa wasanii wa muziki wa Bongo Fleva tu, bali hata wasanii wengine wa sanaa za aina mbalimbali kama vile sanaa za maigizo, filamu na nyinginezo.
Kwa sasa iwapo wakiwa wanatengeneza michezo au filamu zao na kuonekana katika vituo vya luninga vya nchini, ni vema wakatambua kuwa vituo hivyo vimeungana na ving’amuzi mbalimbali na hivyo watakuwa wakitazamwa na nchi za nje.
Suala la ubora wa kazi tena zenye hadhi ya kimataifa ni muhimu kwa kuwa wanawakilisha kimataifa zaidi huku Kiswahili ndio lugha rasmi inayotumika katika kazi zao hizo.
Ni vema wakawa na maudhui yenye mtazamo wa kimaadili na kuweza kukubalika zaidi nje ya nchi. Watengeneze kazi zenye ubora ambao pia unaonesha utalii wa nchi na sio tena maadili mabovu au kuonesha hali ambayo kwa nchini haipo.
Kwa wasanii hao wa sanaa za filamu wanatakiwa pia kuhakikisha kuwa wanawatafuta wataalamu wa lugha na ambao watakuwa wakiwatafsiria vema yale ambayo wanakuwa wakiyazungumza.
Utakuta kuna maneno ya Kiingereza ambayo yanatafsiri kinachozungumzwa na waigizaji yanakosewa na kuweza kuleta aibu sio tu kwao, lakini pia hata kuidharaulisha tasnia nzima kwa ujumla.
Kwa hiyo wasanii wa muziki wa kizazi kipya na hata wale wasanii wa filamu, nao ni vema wakaingia katika changamoto ya kidigitali zaidi ili walikamate soko la nje.
Hata hivyo, changamoto nyingine iliyopo ni kwa wadau wa mawasiliano, waandishi wa habari pamoja na wasanii wenyewe kuhakikisha wanazitazama changamoto katika sekta ya sanaa na kuzitatua haraka iwezekanavyo na kuwatengenezea mazingira bora kwa wasanii hao kunufaika na digitali.


