Wakenya andikeni historia njema uchaguzi wa leo
- Imeandikwa tarehe 04 Machi 2013
- By Gloria Tesha
- Imesomwa mara: 359
LEO ndugu zetu Wakenya takribani milioni 14.3 walioandikishwa kupiga kura mwaka jana na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) ya nchi hiyo, wanatarajiwa kujitokeza kwa wingi kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu unaofanyika leo.
Nchi nyingi huwa zina muda katika uongozi hasa wa juu wa nchi, Kwa upande wao, Wakenya hufanya uchaguzi kila baada ya miaka mitano, na leo watapiga kura kumchagua rais, wabunge na viongozi wengine katika majimbo yote 47.
Utaratibu wa namna ya kupiga kura, umeelezwa na IEBC, ambayo imewataka wapiga kura ambao watakuta hitilafu katika taarifa zao wakati wa kupiga kura, wasihamaki na kuanzisha vurugu, kwani kila mwenye sifa na aliyeandikishwa, atapiga kura.
Miongoni mwa wagombea wa nafasi ya urais wanane katika uchaguzi huo wa taifa hilo lililokumbwa na vurugu mara baada ya matokeo ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2007 na kusababisha vifo vya mamia ya watu, ni wanasiasa na viongozi wakongwe wenye historia za kuvutia katika nchi hiyo.
Katika kampeni, mengi wameahidi na kuyasema, kikubwa kilichonigusa ni namna kila mgombea kwa nafasi yake alivyosisitiza amani, akiwaomba wananchi kutokukubali kuyarudia yaliyotokea mwaka 2008 na kuhakikisha kuwa, hakuna mpiga kura anayepoteza haki yake ya kuchagua.
Aliposimama Uhuru Muigai Kenyatta (Naibu Waziri Mkuu) na mtoto wa Rais wa Kwanza wa Kenya, Jomo Kenyatta, anayewania Urais kupitia Muungano wa Jubilee alisisitiza hayo.
Waziri Mkuu Raila Odinga, mtoto wa aliyewahi kuwa Makamu wa Rais, Jaramogi Oginga Odinga, naye alikazia amani, haki na demokrasia.
Siyo Odinga anayewania Urais kwa Muungano wa CORD na Kenyatta pekee, walioendesha kampeni kali na zenye msisitizo wa amani na utulivu, bali hata wagombea wengine sita wa nafasi hiyo, walisisitiza hilo, akiwemo Naibu Waziri Mkuu mwingine, Musalia Mudavadi, anayewania urais kwa Muungano wa Amani.
Wagombea wengine katika nafasi ya urais katika uchaguzi huo, waliodhihirisha kutotaka ya mwaka 2008 yajirudie ni pamoja na mwana mama pekee Martha Karua wa chama cha NRC, Peter Kenneth wa muungano wa Eagle, Mohamed Abduba Dida wa muungano wa Alliance For Real Change (ARK), Paul Muite wa Safina na Profesa James ole Kiyiapi kupitia Restore and Build Kenya.
Ilikuwa ni nafasi yao wagombea hao kuzungumza waliyoyazungumza ikiwa ni pamoja na kutumia vema kampeni hizo kuomba kura ili wapate ridhaa ya wananchi kuwatumikia katika kipindi cha miaka mitano ijayo.
Binafsi, nikiwa raia wa nchi rafiki na jirani na Kenya, ni wajibu wangu kuwatakia heri ndugu zangu hao katika Uchaguzi huo Mkuu, ambao maelfu ya watu kutoka kila kona ya dunia, wanaelekeza macho na nguvu zao humo kuangalia nini kitajiri na nani ataibuka kidedea.
Baadhi ya wagombea wapo wenye historia zinazovutia na wapo wenye ushawishi mkubwa.
Lakini, wapo waliodhihirisha uwezo mkubwa wa uongozi, hata kama hawana mvuto na wapo walioonekana, wana uchu tu wa madaraka na si uchungu na umasikini unaowakabili asilimia kubwa ya Wakenya.
Yote katika yote, kubwa ni uchaguzi wa leo na matokeo yake. Si vibaya nikasema hili kwamba; wapo baadhi ya mataifa yanayotamani Kenya imwage tena damu ili watekeleze mambo yao.
Lakini, yapo mataifa yanayoombea amani Kenya ikiwemo Tanzania, ili machafuko yasitokee, kwa kile tunachoamini kwamba sisi ni ndugu.
Sasa, itoshe kuwanyamazisha wale wabaya, wanaotamani matokeo mabaya ya uchaguzi nchini Kenya kwa Wakenya kudhihirisha ukomavu wa kisiasa na kuandika historia mpya na njema, itakayofuta na kutusahaulisha machungu yaliyotokea mwaka 2008 baada ya matokeo ya Uchaguzi Mkuu uliofanyika mwaka 2007.
Niwaombe ndugu zangu Wakenya, kuchuja pumba na mahindi, mbivu na mbichi na kutokukubali kutumiwa kwa namna yoyote, hata kama anayeshawishi ni kiongozi wa mkubwa katika jamii.
Wapiga kura wanapaswa kujitokeza kwa wingi na mapema katika vituo vya kura, kama ilivyoelekeza IEBC na kuhakikisha wanazingatia kanuni na utaratibu uliowekwa katika kumchagua kiongozi wanayemtaka.
Mambo yanayokatazwa kwenye vituo vya kupiga kura, leo yazingatiwe na mwenye chokochoko aripotiwe mapema kwa vyombo vya usalama.
Lakini, pia, niwaombe wagombea wa nafasi mbalimbali hasa urais, kutambua kuwa asiyekubali kushindwa si mshindani. Matokeo yatakapotangazwa, wayapokee na kama kuna kutokukubaliana nayo, utaratibu unaozingatia sheria za nchi ufuatwe ili kuzuia lolote baya kutokea.
Wakenya hasa vijana msikubali kushawishiwa kufanya vurugu na mkumbuke atakayewachochea katika hilo, hafai kuwa kiongozi mwema kwa hatima ya maisha yenu na vizazi vijavyo.
Mungu Ibariki Kenya, Mungu Ibariki Afrika. Kila la kheri Wakenya.


