Sita wa familia moja wafa ajalini wakienda harusini Imeandikwa na Na Hellen Mlacky, Same; Tarehe: 19th December 2009 @ 06:51 Imesomwa na watu: 1112; Jumla ya maoni: 5
WATU sita wa familia moja ni miongoni mwa watu 19 waliokufa katika ajali iliyohusisha basi la kampuni ya Mohamed Trans lililogongana uso kwa uso na basi dogo aina ya Asia Combi katika Kijiji cha Kandoto, nje kidogo ya mji wa Same mkoani Kilimanjaro juzi.
Ndugu hao ambao wanatarajiwa kuzikwa leo katika Kijiji cha Mamba Kotela, Moshi Vijijini, walikuwa wakienda katika harusi ya Egbert Maleko iliyotarajiwa kufanyika leo kijijini humo.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Lucas Ng’hoboko, ndugu hao ni pamoja na baba mdogo wa bwana harusi, Geoffrey Maleko (70), ) mkazi wa Mbezi na James Maleko (32) na mtoto wake, Mary James (6), wote wakazi wa Tabata Kisukulu, Dar es Salaam.
Wengine ni Douglas Maleko na mkewe Grace Maleko (47) pia mkazi wa Kisukulu pamoja na baba mdogo wa bwana harusi, Mark Maleko (68) mkazi wa Tabata. Wote wanatarajiwa kuzikwa leo,harusi imeahirishwa.
Aidha, maiti nyingine zilizotambuliwa katika ajali hiyo ni Hevenlight Minja, Neema Minja (13), Witness Minja (10) ambao nao ni ndugu wa familia moja; Glory Makundi mtoto mdogo wa miaka miwili na Johnson Moshi (15) ambaye ni mwanafunzi wa kidato cha kwanza katika Shule ya Sekondari Mabibo.
Wengine waliotambuliwa ni utingo wa basi hilo aliyetambulika kwa jina moja la Simba na mtoto wa Parmina Mandame anayekadiriwa kuwa na miaka 20 hadi 26.
Kamanda huyo wa Polisi alisema hali ya majeruhi watano waliolazwa katika Hospitali ya Wilaya ya Same inaendelea vizuri huku wengine waliolazwa katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC akiwemo fundi wa basi hilo, Hiza Mzungu na Greyson Maleko hali zao bado ni mbaya na wako katika wadi ya uangalizi maalumu (ICU).
Majeruhi wengine ni Sia Maleko (31), Emmanuel Maleko (12), Hawa Dinny (39) mkazi wa Uingereza, Meela Moshi (30), mtawa Valentino Yonas (50), mkazi wa Tanga na Doreen Urio (46) mkazi wa Ilala; ambao wote wamelazwa katika Hospitali ya KCMC.
“Mpaka sasa ni maiti 13 pekee ndio wametambuliwa na ndugu zao na maiti nyingine sita hawajatambuliwa hivyo tunatoa wito kwa wakazi wa Kiimanjaro kujitokeza zaidi ili kuweza kuitabua miili ya ndugu zao,” alisema.
Mganga Mkuu wa Hospitali ya Wilaya ya Same, Charles Kifunde, alisema kati ya majeruhi wote waliopokelewa 35 ambao walikuwa ni abiria wa basi la Mohamed Trans, walipatiwa matibabu na kuruhusiwa juzi kuendelea na safari baada ya kampuni hiyo kuwapa usafiri mwingine.
Aidha, Rais Jakaya Kikwete jana aliwatembelea baadhi ya majeruhi waliolazwa katika Hospitali ya Wilaya ya Same wakiwemo Joseph Akaro, Juta Molel, Waden Abdallah, Julieth Julius na Dorcas Moshi ambaye ni mwanafunzi wa Chuo cha Ualimu Vikindu, Mkuranga na kuwajulia hali.
Ajali hiyo ilitokea juzi Kandoto nje kidogo ya mji wa Same na kuhusisha basi hilo lenye namba T810 AQM na gari dogo lenye namba T845 BCB lenye kufanya safari zake Sinza na Tandika, Dar es Salaam.
Katika hatua nyingine, Jeshi la Polisi nchini limeunda kamati ya watu wanane kwa ajili ya kuchunguza mwenendo mzima wa jinsi mabasi ya Mohamed Trans yanavvyotoa huduma katika mikoa mbalimbali nchini.
Msaidizi wa Kamanda wa Kikosi cha Polisi cha Usalama Barabarani, Mohamed Mtinga alisema hayo jana wakati akizungumza na gazeti hili, alipotakiwa kutoa tamko la jeshi hilo dhidi ya mabasi hayo.
Alisema kamati iliyoundwa inahusisha Jeshi la Polisi pamoja na wadau wengine kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri Majini na Nchi Kavu (Sumatra) ambapo itaongozwa na Kamishna wa Polisi Makao Makuu anayehusika na operesheni, Paul Chagonja na kwamba baadaye watatoa tamko rasmi.
Mabasi ya Mohamed Trans yamekuwa yakipata ajali kubwa na mwaka huu, basi jingine linalofanya safari zake kati ya Dar es Salaam na Nairobi Kenya, liliua abiria 26 katika Kijiji cha Kwakombo, wilayani Korogwe, Mkoa wa Tanga, na mabasi hayo kuzuiwa kwa muda ili yakaguliwe, kabla ya kuruhusiwa kufanya tena safari.