Polisi nchini inashirikiana na Shirika la Polisi la Kimataifa (Interpol) ili kubaini wahusika wa mtandao wa gazeti tando la zeutamu. Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kaimu Msemaji wa Polisi, Juma Said Ally, alisema Polisi inashirikiana na Interpol ili kubaini wamiliki wa mtandao huo.
Alisema wanaamini wahusika wapo ndani na nje ya nchi na hivyo wameamua kushirikiana nao ili kuwakamata na sasa wanaendelea na uchunguzi. “Tunashirikiana na Interpol ili kuwakamata wahusika wanaodhalilisha viongozi na watu mbalimbali na tunaamini wahusika hawa wapo ndani na nje ya nchi, hivyo tunaendelea na uchunguzi,” alisema.
Hatua hiyo ya Polisi kusaka wahusika wa mtandao huo inakuja baada ya wananchi kukerwa na udhalilishaji unaofanywa na wahusika hao kupitia mtandao huo. Siku za karibuni mtandao huo umekuwa ukitumia nafasi ya uhuru wa vyombo vya habari kudhalilisha viongozi, jambo ambalo ni kinyume na maadili ya jamii na uandishi wa habari.
Wakati huohuo, wamiliki wa vyombo vya usafiri wa majini na manahodha wa vyombo hivyo, wametakiwa kuwa na vifaa vya uokoaji ambavyo vitasaidia wanapokumbwa na dhoruba baharini au ziwani. Tahadhari hiyo imetolewa kutokana na majanga ya hivi karibuni mkoani Tanga na juzi majahazi mawili kuzama eneo la Kisiju, Pwani.
Ally alisema jahazi la kwanza liitwalo Dochiwel, lilipigwa na dhoruba na kuzama saa 8 mchana na watu 24 waliokolewa na boti ya Polisi Mv Mamba iliyokuwa ikienda kusaidia uokoaji, ilipata msukosuko baharini na kulazimika kurudi. Aidha, jahazi la Kumekucha lilizama baharini na mizigo iliyokuwa ndani yake saa 12.58 jioni eneo la Mbalukuni, Mafia.
Jahazi hilo lilikuwa likitoka Dar es Salaam likiendeshwa na Khamis Mohamed (35) likiwa limesheheni mifuko 65 ya ngano, mchele mifuko 15, maharage 43, viroba 80 vya sukari, mabati bandari tano na mbao 15 na mabaharia watano ambao walijiokoa.
Katika hatua nyingine, Polisi imesema tuhuma za mafisadi alizozitoa Mwenyekiti Mtendaji wa Kampuni za IPP, Reginald Mengi juzi kudai nchi inahujumiwa na kundi dogo la mafisadi, si mpya kwani baadhi ziko mahakamani na nyingine zipo katika hatua za upelelezi. Ally alimsihi Mengi kama ana jambo jipya aliwasilishe Polisi kwani polisi hawawezi kuzungumzia kesi zilizo mahakamani. Juzi Mengi alizungumza na waandishi wa habari na kuwataja wafanyabiashara watano akidai wameifikisha nchi pabaya na kwamba hawaguswi na serikali.