KLABU ya Simba ya Dar es Salaam imemuengua katika orodha ya wachezaji wake kwa ajili ya Ligi Kuu Tanzania Bara msimu ujao. Habari zilizopatikana ndani ya klabu hiyo jana, zilieleza kuwa jina la Mgosi halipo katika wachezaji waliowasilishwa na timu hiyo kwa ajili ya msimu ujao. Jana ilikuwa mwisho wa timu zote zitakazoshiriki Ligi Kuu Tanzania Bara kuwasilisha usajili wao Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).
“Leo (jana), ndio mwisho wa klabu kuwasilisha usajili wa wachezaji kwa ajili ya Ligi Kuu msimu ujao na sisi (Simba) tumeengua jina la Mgosi, hayupo katika usajili wetu,” kilisema chanzo hicho cha kuaminika. Kulingana na chanzo hicho, Mgosi amekatwa kutokana na kuwepo maelezo kwamba anataka kwenda kufanya majaribio ya kucheza soka ya kulipwa Sweden, hivyo uongozi ukaona ni bora aenguliwe.
Viongozi wa Simba hawakupatikana jana kuzungumzia suala hilo, lakini Mgosi mwenyewe alipoulizwa alisema hana taarifa ya jina lake kuenguliwa. “Ndio kwanza nakusikia kwamba nimeenguliwa, pia hata kama ni kweli nataka kwenda nje huwezi kunikata maana nikishindwa majaribio ina maana sina timu.
“Lakini ngoja nifuatilie nijue kulikoni, ila sina uhakika kama kweli hilo limefanyika,” alisema Mgosi, ingawa chanzo chetu kilituthibitishia kuwa anajua suala la jina lake kukatwa na kwamba mchezaji wa Mtibwa Sugar aliyekuwa amesajiliwa African Lyon kwa ajili ya msimu ujao, Zahoro Pazi ndiye amechukuliwa na Simba kuziba pengo la Mgosi.
Wakati huo huo, Kocha Mkuu wa timu ya Simba, Patrick Phiri, aliwasili Dar es Salaam jana na kupata mapokezi makubwa kutoka kwa mashabiki na baadhi ya wanachama wa timu hiyo.
Mashabiki hao wakiongozwa na kikundi cha ushangiliaji cha timu hiyo cha Muchacho maarufu kama Kidedea, walianza kuwasili Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere kuanzia saa saba mchana na waliendelea kuvuta subira uwanjani hapo hadi majira ya alasiri, kocha huyo alipowasili na kuanza kumshangilia kana kwamba ilikuwa mara ya kwanza kufika nchini.
Akizungumza uwanjani hapo, Phiri raia wa Zambia, alisema amefurahishwa na mapokezi hayo na atawapa mashabiki wa Simba kile wanachokitaka, ambacho ni ushindi kwa timu yao.
“Sijawahi kupata mapokezi kama haya, nimejisikia furaha sana, nawahakikishia mashabiki wa Simba nitajitahidi kuwapa raha,” alisema Phiri na kuongeza kuwa ana matumaini kikosi kilichosajiliwa kitakuwa imara na kitarudisha heshima ya Simba katika michuano ya ndani na kimataifa.
Akizungumzia kuhusu kuchelewa kuja nchini, kocha huyo alisema ni kutokana na kuwa na matatizo binafsi na kwamba haikuwa dhamira yake kuchelewa kuja kuinoa timu hiyo. Phiri aliyejiunga Simba mwanzoni mwa duru la pili la Ligi Kuu Tanzania Bara, alienda kwao kwa mapumziko baada ya ligi kumalizika mwezi Aprili na alitarajiwa kurejea nchini mwishoni mwa mwezi uliopita, lakini alishindwa kufanya hivyo.