MWENGE wa Uhuru unaendelea na mbio zake na sasa upo mkoani Tanga, ambapo unatarajiwa kukimbizwa kwenye halmashauri 11 na kuzindua miradi 82 yenye thamani ya zaidi ya Sh bilioni 33.
Akizungumza leo Alhamisi Mei 26, 2022, wakati wa makabidhiano ya Mwenge wa Uhuru, ambao umetokea Zanzibar, Mkoa wa Mjini Magharibi, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Adam Malima amesema utakimbizwa Kilometa 1,834.3 katika halmashauri 11 za Mkoa huo.
Alizitaja hamashauri hizo kuwa ni Tanga Jiji, Mkinga, Muheza, Pangani, Handeni Wilaya, Kilindi, Handeni Mji, Korogwe Wilaya, Bumbuli, Lushoto na Korogwe Mji.
Amesema miradi itakayozinduliwa, kuwekewa mawe ya msingi na kutembelewa ipo katika sekta za elimu, afya, barabara, maji, miradi ya kiuchumi na kijamii.