Mpaka Hifadhi ya Ruaha warekebishwa

SPIKA wa Bunge, Dk Tulia Ackson amesema makubaliano kuhusu uwekezaji wa bandari hayana tatizo hivyo wananchi wasiwe na wasiwasi. Dk Tulia amesema Bunge limeridhia makubaliano kati ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Dubai na si mkataba kwa kuwa haupo.

Alisema hayo Dodoma jana asubuhi wakati akizungumza katika kipindi cha Jambo Tanzania kilichorushwa na kituo cha TBC1 cha Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC).

Dk Tulia alisema serikali imeingia makubaliano na serikali ya Dubai katika ushirikiano wa kuendeleza bandari kupitia kampuni ya DP World na Juni 10, mwaka huu Bunge liliridhia makubaliano hayo na si mkataba.

“Yale ni makubaliano sio mkataba, kwanini imekuja bungeni kwa sababu katiba inataka hivyo maana aina ya makubaliano haya yanataka chombo ambacho nchi imekipa madaraka ya kuridhia,” alisema.

Aliongeza: “Sisi tumevipitia vifungu kimoja baada ya kingine na sisi kama wawakilishi wa wananchi tumejiridhisha vifungu vile havina shida yoyote sababu vinaipa nafasi serikali kuingia kwenye majadiliano ambayo baadaye yatapelekea mkataba.”

Dk Tulia alisema makubaliano hayo hayakuzungumzia suala la muda kwa sababu yameweka msingi tu hivyo si rahisi kufahamu ni lini Tanzania na Dubai zitakuwa zimemaliza jambo fulani.

“Huwezi kusema ndani ya muda huu tutakuwa tumemaliza, umemaliza nini, tulikuwa sahihi kupitisha na hakuna tatizo…mfano wa pili ambao watu wanalalamika bandari zetu zote zitachukuliwa, hapana.

Haya makubaliano lazima waseme wataanzia wapi mpaka wapi na akija mwekezaji mwingine mwenye ofa analeta mezani dau kubwa zaidi hawalazimiki kumpa huyu (DP World) sijui watu hili neno lazima wanalitoa wapi,” alisema.

Dk Tulia alisema si busara wananchi kuchukulia suala hilo kisiasa kwa kuwa ni jambo la maendeleo ya nchi na maendeleo.

“Kama mkataba ukishasainiwa kisha kwenye utekelezaji wake tukaona kuna shida, sheria inaruhusu bunge kuita mkataba ukaja tukajadili…kama mambo yatakwenda sivyo tuwajibike hapana, tutaiwajibisha serikali kwa maana ya kwamba mimi binafsi au bunge kuwajibika sioni mazingira gani sababu aina ya makubaliano yaliyoletwa bungeni sioni madhara yoyote,” alisema.

Ripoti za CAG Kuhusu kufanyia kazi ripoti za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Dk Tulia alisema Bunge linazifanyia kazi na si kweli kwamba halina meno. Ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa kutoa ushirikiano wa mabadiliko yaliyofanywa na bunge kwenye kuzifanyia kazi ripoti hizo.

Habari Zifananazo

1 Comment
Oldest
Newest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
Back to top button